Zelensky ajitolea kujiuzulu ili Ukraine ipate uanachama NATO
24 Februari 2025Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema jana Jumapili -- siku moja kabla ya kumbukumbu ya miaka mitatu ya uvamizi wa Urusi – kuwa yuko tayari kujiuzulu kama kiongozi wa nchi hiyo iwapo hatua hiyo itairuhusu Ukraine kupokelewa katika muungano wa kijeshi wa NATO.
Soma: Mabadiliko ya kimataifa kuamua awamu mpya ya vita Ukraine
Zelensky ambaye amekabiliwa na ukosoaji mkubwa kutoka utawala mpya wa Marekani, ameeleza kuwa angetaka kukutana na Donald Trump kabla ya rais huyo wa Marekani kukutana na mwenzake wa Urusi, Vladimir Putin.
Zelensky amekuwa akishinikiza Ukraine kupewa uanachama wa NATO kama sehemu ya makubaliano yoyote ya kumaliza vita, lakini muungano huo unaoongozwa na Washington umekuwa na tahadhari kuhusu ombi hilo.
Trump na Zelensky wamekuwa wakirushiana maneno tangu maafisa wa Marekani na Urusi walipokutana wiki iliyopita nchini Saudi Arabia kwa mazungumzo ya ngazi ya juu kwa mara ya kwanza katika muda wa miaka mitatu.