MigogoroUlaya
Wawakilishi wa Urusi na Ukraine wanakutana Istanbul
16 Mei 2025Matangazo
Matarajio ya kupatikana mwafaka kwenye mazungumzo hayo ni madogo hasa baada ya Rais Vladimir Putin kukataa wito wa mwenzake wa Ukraine Volodymyr Zelensky wa kufanya mkutano wa ngazi ya marais nchini Uturuki.
Badala yake Putin ambaye ndiye alitoa pendekezo la mazungumzo hayo, ameutuma ujumbe wa ngazi ya chini unaoongozwa na mshauri wake wa masuala ya siasa.
Hayo yatakuwa mazungumzo ya kwanza ya ana kwa ana kati ya pande hizo mbili tangu yalipovunjika mengine yaliyofanyika Uturuki mnamo wiki za mwanzo za uvamizi wa Urusi nchini Ukraine mwaka 2022.
Kyiv iliondoka kwenye mazungumzo hayo ya awali ikipinga matakwa ya Urusi ikiwemo kuilazimisha iachane na mipango ya kujiunga na Jumuiya ya Kujihami ya NATO pamoja na kupunguza ukubwa wa jeshi lake.