Watu saba wauawa baada ya madaraja mawili kulipuliwa Urusi
1 Juni 2025Matukio hayo yamejiri kabla ya mazungumzo yanayopangwa ya amani yenye lengo la kumaliza vita vilivyodumu kwa miaka mitatu nchini Ukraine.
Soma pia:Makabaliano ya Urusi na Ukraine yasababisha vifo na majeruhi
Wapelelezi wa Urusi wamesema daraja la barabara kuu lililoko juu ya reli katika mkoa wa Bryansk lililipuliwa Jumapili saa tano kasoro dakika kumi usiku wakati treni iliyokuwa imebeba abiria 388 kuelekea Moscow ilikuwa inapita chini yake. Saa nne baadae, daraja la reli lililoko juu ya barabara kuu lililipuliwa katika eneo jirani la Kursk. Vipande treni ya mizigo vilizagaa barabarani kufuatia tukio hilo.
Kamati ya uchunguzi ya Urusi, ambayo huchunguza matukio makubwa ya uhalifu, iliyahusisha matukio hayo na kusema kwa uwazi kwamba madaraja yote mawili yalilipuliwa. Wapelelezi wa Urusi wamesema ni vtendo vya ugaidi.
Ukraine mpaka sasa haijatoa taarifa yoyote kuhusu matukio hayo mawili. Wajumbe wa Urusi na Ukraine wanatarajiwa kukutana Jumatatu mjini Istanbul kwa duru ya pili ya mazungumzo ya moja kwa moja ya kujadili namna ya kumaliza vita.