Wanaharakati Kenya waandamana kupinga kesi dhidi ya Besigye
24 Februari 2025Mashirika ya kiraia nchini Kenya na mengine ya kimataifa yamefanya maandamano ya amani hii leo ya kupinga kushikiliwa kwa wafungwa kinyume cha sheria na utekaji nyara wa kiongozi wa upinzani wa Uganda, Kizza Besigye.
Mashirika hayo yamesema serikali ya Rais Museveni inakiuka utawala wa sheria kwa kuwazulia mahasimu wake wa kisiasa. Mashirika hayo, yakiwemo Amnesty International, Muungano wa Madaktari, Wafamasia na Madaktari wa Meno wa Kenya (KMPDU), Vocal Africa na Tume ya Kimataifa ya Wanasheria (ICJ) yaliwasilisha ombi kwa Bunge la Taifa likitaka vyombo vya usalama kuwajibika.
Soma: Uganda yahamisha kesi ya Besigye katika mahakama ya kiraia
Ombi hilo, lililowasilishwa kwa Kamati ya Bunge ya Ulinzi, Ujasusi na Mahusiano ya Kigeni, linatoa wito wa kufanyika kwa uchunguzi kuhusu madai ya utekaji nyara na usafirishaji haramu wa Besigye na mwenzake, Hajj Obeid Lutale. Baadaye walielekea hadi kwenye ubalozi wa Uganda ambapo waliwasilisha ombi la kuachiliwa kwa wafungwa wa kisiasa nchini Uganda bila ya masharti.
Wito wa kuachiliwa kwake umeendelea kuongezeka, huku Wakenya na Waganda wakijumuika mitandaoni chini ya alama ya reli #FreeKizzaBesigye.