Viongozi wa dini waeneze amani kuelekea uchaguzi
20 Agosti 2025Kongamano hilo ambalo pia limehudhuriwa na viongozi wa dini, wanasheria pamoja na wanasiasa linafanyika kama sehemu ya kujenga daraja litakalofanikisha uchaguzi mkuu ambao kwa mujibu wa tume huru ya taifa ya uchaguzi INEC utafanyika Oktoba 29.
Uchaguzi wa mwaka huu utafanyika kwa wakati mmoja kuanzia ngazi ya madiwani, wabunge na rais na kwamba tayari baadhi ya vyama vya siasa vimeshaanza kuwasambaza wagombea wake ilihali chama tawala CCM kimeanza vikao vya kupitia majina ya wagombea wa ubunge.
Mwaka mmoja tangu kutoweka kwa wanaharakati wa CHADEMA
Pamoja na kujitokeza hoja mbalimbali ndani ya kongamano hilo linalofanyika kwa mara ya kwanza tangu kupulizwa kipyenga cha uchaguzi wenyewe, suala la amani na utulivu wakati wote wa uchaguzi ni mada iliyopewa nafasi kubwa kwa kila mjumbe aliyepanda jukwaani kuzungumza.
Vyombo vya maamuzi vyaombwa kutenda haki
Vyombo vya maamuzi ikiwamo, tume huru ya taifa ya uchaguzi, ofisi ya msajili wa vyama vya siasa pamoja na jeshi la polisi walikumbushwa namna wanavyopaswa kutenda haki na kwamba utekelezaji wa majukumu yao kwa weledi ni sehemu ya karata muhimu kufanilkisha uchaguzi huo.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya maridhiano, jumuiya ambayo ndiyo iliyoandaa kongamano hilo, Alhadi Mussa Salumu alisema katika nasaha zake kuwa mkutano huo haukulenga kupiga porojo, bali kujadili, kuainisha na kupanga mikakati ya namna ya kuhifadhi amani ya nchi wakati huu wa kuelekea uchaguzi mkuu.
Taasisi za kiserikali na zile zisizo za kiserikali ni sehemu ya washiriki wa kongamano hilo ambalo pia limewakaribisha baadhi ya wajuzi wa masuala ya dini kutoka nchini Kenya.
Sheikh Juma Ngao wa Jukwaa la KEMNAC nchini Kenya alisema hakuna kitabu cha dini kinachohimiza chuki wala utengano hivyo aliwasihi wananchi wa Tanzania kuendelea kuthamini dhima waliyoridhishwa na amani na tulivu.
Jeshi la polisi lasisitiza linatekeleza majukumu yake kwa weledi
Kwa upande mwingine ingawa mara kwa mara jeshi la polisi limekuwa likinyooshewa kidole na wanasiasa pamoja na waandishi wa habari kwa namna ivyoshughulikia mikutano ya wanasiasa, jeshi hilo limesisitiza kutekeleza majukumu yake kwa weledi na haki.
Kamanda wa kanda maalumu ya Dar es Salaam aliyezungumza katika kongamano hilo, kamanda Jumanne Muliro alionya kuwa uchaguzi isichukuliwe kuwa kigezo kwa raia kuvunja sheria.
Lissu akutwa na kesi ya kujibu kuhusu uhaini
Alisema jeshi la polisi litaendelea kutekeleleza majumu yake kama ilivyo desturi ikiwamo kuwasaka wale wanaoashiria kusababisha uvunjifu wa amani.
Watanzania wanatarajia kuteremka katika vituo vya kipigia kura Oktoba 29, huku baadhi ya wanasiasa wakiwa wamegawika wakiwamo wale wanaopinga uchaguzi huo hadi pale kutakapofanyika mageuzi ya uchaguzi, wakati wengine wakisisitiza kujitokeza kwa wingi siku ya kura.