ASEAN yakubaliana kuukabili Ushuru wa Trump
27 Mei 2025Viongozi wa mataifa ya Kusini Mashariki mwa Asia yaliko kwenye jumuiya ya ushirikiano yaASEAN, wamekubaliana kuchukuwa msimamo wa pamoja kuhusu namna ya kushughulikia suala la ushuru wa kibiashara wa Marekani.
Hayo yameelezwa na Waziri Mkuu wa Malaysia, Anwar Ibrahim ambaye ni mwenyekiti wa sasa wa jumuiya hiyo.
Akizungumza kwenye mkutano na waandishi habari amesema viongozi wa jumuiya hiyo wamekubaliana kufuata msimamo wa pamoja utakaohakikisha hakuna nchi itakayoumia peke yake kutokana na ushuru wa Marekani na kwa pamoja zitaendelea na mazungumzo ya kibiashara na Washington.
Kadhalika viongozi hao wanaokutana katika mkutano wao wa kilele mjini Kuala Lumpur, wametoa mwito kwa pande zote zinazozozana nchini Myanmar kurefusha makubaliano ya usitishaji vita na kujenga hali ya kuaminiana kuelekea mazungumzo ya kitaifa.