Urusi na Ukraine zashambuliana usiku kucha
8 Juni 2025Urusi imefanya mashambulizi katika eneo la kati la Ukraine usiku wa kuamkia leo na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kufanya uharibifu mkubwa wa mali, maafisa nchini humo wamesema.
Mkoa wa viwanda wa Dnipropetrovsk umeshambuliwa kwa droni, mizinga na maroketi, ambapo miundombinu yake imeharibiwa.
Kwa upande mwingine, Ukraine nayo imefanya mashambulizi katika mji mkuu wa Urusi, Moscow, na kupelekea kufungwa kwa viwanja viwili vya ndege , mamlaka ya Urusi imesema mapema hii leo.
Wikiendi hii nchi hizo zilipanga kufanya mabadilishano ya wafungwa lakini Moscow imeishutumu Ukraine kwa kutokubali tarehe ya mabadilishano, wakati Kyiv ikisema Urusi inacheza "mchezo mchafu" kwa kutozingatia vigezo vilivyokubaliwa.
Mashambulizi baina ya pande hizo mbili yameongezeka huku mazungumzo ya mjini Istanbul yakishindwa kusuluhisha vita hivyo vilivyodumu kwa zaidi ya miaka mitatu.