UN yasema kundi la M23 limetenda uhalifu wa kivita DR Kongo
6 Septemba 2025Ripoti ya Umoja wa Mataifa imebainisha kuwa majeshi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na waasi wa kundi la M23 wamekiuka haki za binadamu kwa kiwango kikubwa katika mgogoro unaoendelea nchini Kongo.
Umoja wa Mataifa umesema katika ripoti hiyo kwamba huenda pande mbili hizo zimetenda uhalifu wa kivita.
Kamishna wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia Haki za Kibinadamu, Volker Türk, ameelezea ukatili uliobainishwa katika ripoti hiyo kuwa ni wa kutisha. Hii ni mara ya kwanza kwa Umoja wa Mataifa kutamka kuwa uhalifu wa kivita umetendeka katika mgogoro wa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Umoja huo umesema waasi wa M23 wamewaua watu kiholela, wamewatesa na pia wamewateka watu nyara. Kulingana na ripoti hiyo, kundi hilo pia lilitenda unyanyasaji wa kijinsia kwa makusudi, ikiwa ni pamoja na ubakaji wa magenge, hasa dhidi ya wanawake kwa nia ya kudhalilisha, kuadhibu, na kuuvunja utu wa waathiriwa.