Ujerumani yasema vifo huko Gaza vinatia wasiwasi mkubwa
24 Machi 2025Ujerumani imesema ina wasiwasi mkubwa kutokana na kuongezeka kwa vifo vya raia katika Ukanda wa Gaza tangu Israel ilipoanzisha upya mashambulizi yake ya kijeshi katika ukanda wa huo.
Israel ilianzisha tena mashambulizi ya anga siku ya Jumanne wiki iliyopita yaliyofuatiwa na operesheni ya ardhini baada ya kuyavunja makubaliano ya wiki sita ya usitishaji wa vita kati yake na kundi la Hamas ambalo linaitawala Gaza.
Soma pia: Ujerumani yaihimiza Israel kuondoa vikwazo vya misaada Gaza
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani Christian Wagner amesema hali ya kibinadamu huko Gaza kwa mara nyingine tena imerudi kuwa janga na ametoa mwito kwa pande zote mbili kurejea katika meza ya mazungumzo na kusitisha mapigano.
Ujerumani pia imelaani uamuzi wa Israel wa kuyatambua maeneo mapya yanayokaliwa kimabavu na walowezi wa Kiyahudi katika Ukingo wa Magharibi, imesema kwamba hatua hizo zinadhoofisha juhudi za kufikiwa kwa suluhisho la kuanzishwa kwa mataifa mawili huru ya Israel na Palestina.