Uingereza yajitolea kwa ajili ya amani ya kudumu Ukraine
4 Machi 2025Haya yamesemwa na serikali ya nchi hiyo baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kusitisha kwa muda msaada wake wa kijeshi kwa Ukraine. Msemaji wa serikali ya Uingereza amesema kuwa bado wamejitolea kwa amani ya Ukraine na kuongeza kuwa ndilo jambo sahihi la kufanya.
Wakati huo huo, Rais wa Halmashauri Kuu ya Umoja wa Ulaya Ursula von der Leyen, leo amependekeza ufadhili mpya wa takriban dola bilioni 841.5 kwa uwekezaji wa ulinzi katika umoja huo pamoja na msaada wa kijeshi kwa Ukraine.
Soma pia: Keir Starmer awahimiza viongozi wa Ulaya kusimamia usalama wao
Shinikizo la kuongeza ufadhili kwa Ukraine limeongezeka dhidi ya umoja huo baada ya tangazo hilo la Trump la kukatiza msaada kwa Ukraine.
Huku hayo yakijiri, ikulu ya Urusi ya Kremlin imesema kuwa kukatizwa kwa msaada wa Marekani kwa Ukraine ni mchango bora zaidi kwa amani.