Trump: Vita vya biashara vitawaumiza Wamarekani
3 Februari 2025Rais wa Marekani, Donald Trump, ameagiza vikwazo vya ushuru kwa bidhaa zinazoingizwa kutoka Canada, Mexico, na China. Kwa hatua hizi, bidhaa kutoka Mexico na Canada zitatozwa ushuru wa asilimia 25, na bidhaa kutoka China zitakabiliwa na ushuru wa asilimia 10.
Waziri Mkuu wa Canada, Justin Trudeau, amejibu hatua hiyo kwa kutangaza ushuru wa asilimia 25 kwa bidhaa za Marekani. Mexico, Canada, na China ni washirika wakubwa watatu wa biashara wa Marekani kwa mpangilio huo, na kwa pamoja wanajumuisha zaidi ya asilimia 40 ya biashara ya jumla ya bidhaa.
Ofisi ya Trudeau ilisema katika taarifa kuwa waziri mkuu huyo na Rais wa Mexico, Claudia Sheinbaum, walijadili utekelezaji wa ushuru huo kwa njia ya simu, na kukubaliana kushirikiana katika maeneo ya maslahi ya pamoja na kuendelea kuimarisha uhusiano baina ya mataifa yao.
"Tulizungumza kuhusu utekelezaji wa ushuru wa Marekani kwa nchi zote mbili, pamoja na juhudi zao za kuboresha usalama wa mipaka na kupambana na uzalishaji na usambazaji wa dawa za kulevya haramu," taarifa ilisema.
Soma pia: China yaapa kulinda maslahi yake baada ya kitisho cha ushuru kutoka kwa Trump
Tofauti na Mexico, ambapo rais wake ametangaza tu utekelezaji wa ushuru wa kulipiza kisasi bila kubainisha kiwango au bidhaa yoyote, Trudeau ametangaza kwamba Canada itajibu kwa kuweka ushuru wa asilimia 25 kwa bidhaa za Marekani zenye thamani ya dola bilioni 255.
Trump akiri ushuru wake unaweza kuwaumiza Wamarekani
Rais Trump alisema Jumapili kwamba ushuru mkubwa alioutangaza dhidi ya bidhaa kutoka Mexico, Canada, na China unaweza kusababisha "maumivu fulani" kwa Wamarekani, huku Wall Street na washirika wakubwa wa kibiashara wa Marekani wakionyesha matumaini kwamba vita vya biashara havitadumu kwa muda mrefu.
Trump, ambaye alianza muhula wake wa pili kama rais Januari 20, alanzisha ushuru alioutangazia Jumamosi. Wakosoaji walisema hatua dhidi ya washirika watatu wakubwa wa kibiashara wa Marekani zitawaumiza Wamarekani kwa kuongeza bei na kupunguza ukuaji wa uchumi duniani.
Trump alitetea uamuzi wake kwenye mitandao ya kijamii Jumapili, akisema "Marekani ina deni kubwa kwa Canada, Mexico, na China (na karibu nchi zote!), inadaiwa Dola Trilioni 36, na hatutakuwa 'nchi pumbavu' tena," aliandika rais huyo kutoka chama cha Republican.
Soma pia: Je, EU inaanzisha vita vya biashara na China
Akizungumza kwa herufi kubwa, Trump aliongeza, "Hii itakuwa enzi ya dhahabu ya Amerika! Je, kutakuwa na maumivu fulani? Ndio, labda (na labda sivyo!)." Trump hakufafanua alichomaanisha kwa "maumivu fulani."
Masoko ya kifedha yalikuwa yamefungwa mwishoni mwa wiki lakini hatua hizo zitahisiwa mara moja wakati biashara ya hisa za Marekani itakapoanza Jumatatu saa 6 usiku. Masoko yalikuwa yakisubiri hatua hizo kwa wasiwasi, lakini wachambuzi wengine walisema kulikuwa na matumaini ya majadiliano, hasa na Canada na China.
"Kwa siku mbili tu kabla ya utekelezaji, inaonekana ushuru utaanza kutumika, ingawa makubaliano ya dakika za mwisho hayawezi kuondolewa kabisa," walisema wataalamu wa uchumi wa Goldman Sachs kwenye noti yao Jumapili.
Soma pia: Jimbo la 51 la Marekani? Jinsi Canada inavyoweza kumkabili Donald Trump
Waliongeza kuwa kwa sababu Ikulu ya White House iliepuka kuweka masharti maalum ya kuondoa ushuru, ushuru huo unaweza kuwa wa muda mfupi, "lakini mtazamo bado haujulikani."
Ushuru wa Trump, ulioainishwa katika amri tatu za utendaji, unatarajiwa kuanza kutumika saa siku ya Jumanne. Trump aliahidi kuuweka hadi pale kile alichokiita dharura ya kitaifa kuhusu fentanyl, opioid hatari, na uhamiaji haramu kwenda Marekani itakapomalizika.
China iliiweka milango wazi kwa mazungumzo na Marekani. Upinzani wake mkali ulikuwa kuhusu fentanyl. "Fentanyl ni tatizo la Marekani," ilisema wizara ya mambo ya nje ya China, ikiongeza kwamba China imechukua hatua kubwa kupambana na tatizo hilo.
Uchunguzi wa Reuters/Ipsos uliofanywa wiki iliyopita unaonyesha kwamba Wamarekani waligawanyika kuhusu ushuru, ambapo asilimia 54 walipinga ushuru mpya kwa bidhaa zinazoingizwa na asilimia 43 walikuwa wanauunga mkono, huku Wademocrat wakipinga zaidi na Republicans wakimunga mkono zaidi.
Kitisho cha ushuru dhidi ya jumuiya ya BRICS
Rais Trump amekuwa akitishia mara kwa mara nchi wanachama wa BRICS kwamba ataweka ushuru wa asilimia 100 kwa bidhaa zao zinazokuja Marekani ikiwa wataendelea na juhudi zao za kuanzisha sarafu ya hifadhi itakayoshindana na dola ya Marekani.
Kundi la BRICS linaitwa kwa vifupisho vya majina ya mataifa wanachama wake wa awali - Brazil, Urusi, India, China na Afrika Kusini. Nchi hizi zinajaribu kupunguza utegemezi wao kwa dola ya Marekani, sarafu ya hifadhi duniani, inayotumika katika karibu asilimia 80 ya biashara ya kimataifa.
Soma pia: China yahadharisha juu ya kuporomoka biashara ulimwenguni
Wataalamu wengi wa uchumi wanakubaliana kwamba mfumo wa kifedha unaotawaliwa na dola unatoa faida kubwa kwa Marekani kiuchumi, ikiwemo gharama za mkopo za chini, uwezo wa kudumisha upungufu mkubwa wa bajeti na utulivu wa viwango vya kubadilishana, miongoni mwa mengine.
Rais wa Urusi Vladmiri Putin na kiongozi wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva ndio wafuasi wakubwa wa sarafu mpya. Wakati China haijaeleza wazi msimamo wake, Beijing imeunga mkono mipango ya kupunguza utegemezi kwa dola. India, kwa upande mwingine, inachukuwa tahadhari zaidi kuhusu wazo hilo.
Je, EU inapaswa kuhofia vita vya kibiashara na Marekani?
Katika kampeni zake, Donald Trump alijikita sana juu ya China, lakini pia aliuita Umoja wa Ulaya "China ndogo." Mwishoni mwa Oktoba, alionya kuwa umoja huo utalipa mwishowe na akaahidi kupitisha "Sheria ya Biashara ya Kurudisha ya Trump."
"Hawachukui magari yetu. Hawachukui mazao yetu ya kilimo. Wanauza mamilioni ya magari hapa Marekani," alisema kwenye mkutano wa hadhara huko Pennsylvania. "Hapana, hapana, hapana. Watapaswa kulipa gharama kubwa."
Serikali ya Trump inapendekeza sera za kiuchumi zitakazoshughulikia changamoto kubwa kwa Umoja wa Ulaya, na hasa kwa Ujerumani, wataalamu wanasema.
Soma pia: Von der Leyen: Siku zijazo Ulaya huenda zikawa ngumu
Taasisi ya Ifo imekokotoa kuwa ushuru wa asilimia 20 kwa bidhaa zinazouzwa kutoka nje unaweza kusababisha mauzo ya Ujerumani kwa Marekani kupungua kwa takribani asilimia 15 na kusababisha hasara ya kiuchumi ya €33 bilioni ($35.3 bilioni).
Taasisi ya Uchumi ya Ujerumani yenye makao yake mjini Cologne imekadiria kuwa vita vya kibiashara vyenye ushuru wa asilimia 10 pande zote mbili vinaweza kugharimu uchumi wa Ujerumani €127 bilioni kwa kipindi cha miaka minne cha utawala wa Trump. Ushuru wa asilimia 20 unaweza kuugharimu uchumi wa Ujerumani €180 bilioni.
Mgogoro wa ushuru kati ya Marekani na Umoja wa Ulaya unaweza pia kuwa tatizo kwa uchumi wa Marekani. Ushuru usiochokozwa wa Marekani bila shaka utasababisha kisasi kwa njia ya ushuru wa majibu. Hii itafanya bidhaa za Ulaya kuwa ghali zaidi kwa watumiaji wa Marekani, kuongeza bei kwa ujumla na kuchangia ongezeko la bei.
Chanzo: rtre, dw