Trump achukizwa na mashambulizi ya Israel huko Qatar
10 Septemba 2025Rais wa Marekani Donald Trump amesema hajafurahishwa na hatua ya Israel ya kuwashambulia maafisa wa Hamas nchini Qatar jana Jumanne. Kama ilivyo kwa Israel, Qatarnayo ni mshirika wa karibu wa Marekani na ndio mpatanishi muhimu katika mazungumzo baina ya Israel na Hamas katika kutafuta njia ya kufikia mwisho vita huko Gaza.
"Sijafurahishwa , sifurahishwi na hatua hiyo. Sina haja ya kufanya hivyo. Sijafurahishwa na hali nzima. Sio hali nzuri. Lakini, nitasema hivi. Tunataka mateka warudi. Lakini hatujafurahishwa na kilichotokea."amesema Trump.
Trump ameongeza kwamba uamuzi huo ulifanywa na Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu na kwamba Marekani haikushirikishwa katika mipango ya shambulizi hilo.
Mataifa mengine ikiwemo China, Ujerumani na Ufaransa yameelezea pia wasiwasi wao kuhusu tukio hilo yakilitaja kwamba halikubaliki.