Serikali ya Uholanzi yaanguka baada ya kujiondoa kwa PVV
3 Juni 2025Katika ujumbe aliochapisha kwenye mtandao wa kijamii wa X, Wilders amesema, ''hakuna ridhaa kwa mipango yetu ya hifadhi, PVV inajiondoa kwenye muungano'' akimaanisha chama chake cha mrengo mkali wa kulia.
Wildersameongeza kusema kuwa amemjulisha waziri mkuu kwamba atawaondoa mawaziri wa PVV kwenye baraza la mawaziri na kwamba hawawezi tena kubeba jukumu kwa hilo.
Kilichomghadhabisha Wilders
Wilders ameghadhabishwa na kile alichokiona kama kasi ndogo ya kuanzisha sera kali zaidi ya uhamiaji iliyokubaliwa na washirika wa muungano baada ya ushindi wake wa kushangaza katika uchaguzi wa Novemba mwaka 2023.
PVV bado ina ushawishi zaidi
Miezi kumi na minane baada ya ushindi wake huo ulioleta mshtuko kote Ulaya, kura za maoni zinaonyesha kuwa chama chake cha PVV bado ndicho chenye ushawishi zaidi.
Mazungumzo ya dakika za mwisho kuhusu mzozo huo leo asubuhi, yalichukuwa takribani nusu saa kabla ya viongozi wa vyama vinne vya muungano kutoka wakiwa katika hali ya kukasirika.
Hatua ya Wilders yatajwa kuwa ukosefu wa uwajibikaji
Kiongozi wa chama cha kiliberali cha VVD, Dilan Yesilgoz, aliyeonekana kuwa na hasira, ameitaja hatua ya Wilders kuwa ya ukosefu mkubwa wa uwajibikaji na akaongeza kuwa anahofia itatoa fursa kwa vyama vya mrengo wa kushoto.
Mchakato wa Wilders kutafuta washirika Uholanzi wavurugika
Kujiondoa kwa chama hicho cha PVV kutoka kwenye serikali hiyo ya muungano, kunafungua kipindi cha kukosa uhakika wa kisiasa katika taifa hilo la tano lililoimarika kiuchumi barani Ulaya ambalo pia ni muuzaji mkubwa wa bidhaa nje ya nchi, huku vyama vya mrengo mkali wa kulia vikipata mafanikio katika bara zima.
Chama cha siasa kali Uholanzi chajipanga kuunda serikali
Hatua hiyo pia inakuja wiki chache kabla ya Uholanzi kuwa mwenyeji wa viongozi wa ulimwengu kwa mkutano wa kilele wa jumuiya ya kujihami ya NATO.
Pia inaweza kuchelewesha uamuzi juu ya uwezekano wa kihistoria wa kuongezwa kwa matumizi ya ulinzi ili kufikia malengo mapya ya NATO.