Ramaphosa aapa kutoitupa mkono Kongo
3 Februari 2025Wanajeshi 14 wa Afrika Kusini pamoja na wengine kutoka nchini Malawi na Tanzania waliuawa kwenye makabiliano na kundi la M23 linalopambana na serikali ya Kongo na ambalo limefanikiwa kusonga mbele mashariki mwa nchi hiyo katika wiki za karibuni.
Taarifa iliyotolewa na ikulu mjini Pretoria imemkariri Ramaphosa akisema kwamba Afrika Kusini haitowatupa mkono watu wa Kongo na kuongeza kwamba amani ya kudumu mashariki mwa nchi hiyo na kanda nzima itapatikana kwa mshikamano na mataifa mengine.
Soma pia:Kongo yazitaka timu za ulaya kusitisha ufadhili kwa Rwanda
Matamshi ya Ramaphosa yanafuatia miito kutoka kwa wanasiasa vigogo wa Afrika Kusini ya kuitaka serikali iwaondoe wanajeshi wake kutoka Kongo waliopelekwa chini ya kikosi cha kulinda amani kinachofadhiliwa na Jumuiya ya SADC.